Na LEONARD ONYANGO
MBUNGE wa Lugari Ayub Savula amedhihirisha wazi ukweli kwamba wanasiasa ni vigeugeu – hawana tofauti na kinyonga anayebadili rangi kulingana na mazingira.
Mbunge huyo ambaye alichaguliwa kwa mara ya kwanza mnamo 2013, aliwaacha wafuasi wake vinywa wazi baada ya kumtoroka kiongozi wa chama chake cha Amani National Congress (ANC) Musalia Mudavadi, na kufululiza hadi nyumbani kwa Katibu Mkuu wa Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi (Cotu) Francis Atwoli anayeunga mkono kinara wa ODM Raila Odinga.
Tamasha
Majuzi tu Bw Savula alikuwa miongoni mwa viongozi wa ANC walioandamana na Bw Mudavadi katika Tamasha za Kitamaduni za Jamii ya Maragoli mjini Mbale, Kaunti ya Vihiga.
Ni katika tamasha hizo ambapo Seneta wa Kakamega Cleophas Malala alitishia kuvuruga mkutano uliofanyika Ijumaa katika uwanja wa Bukhungu, Kaunti ya Kakamega, kabla ya kuonywa na polisi.
Lakini kabla ya tamasha hizo kumalizika, Bw Savula aliongoza kundi la wanasiasa na kufululiza hadi nyumbani kwa Bw Atwoli katika eneo la Khwisero, Kakamega, na kuomba msamaha.
Siku ya Ijumaa Savula alihudhuria mkutano wa Azimio la Umoja wa Magharibi ugani Bukhungu Kakamega na kutangaza kuhama OKA.