NA CHARLES WASONGA
UKOSEFU wa uongozi thabiti ndani na nje ya bunge ndio chimbuko la misukosuko inayotishia kusambaratisha muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya, wadadisi wa masuala ya kisiasa sasa wanasema.
Wanasema kuwa kujivuta kwa mwenyekiti wa Baraza Kuu la muungano huo rais mstaafu Uhuru Kenyatta kuitisha mkutano wa uongozi wa chama hicho ili kutoa mwelekeo na msimamo wa muungano huo kuhusiana na masuala mbalimbali ya kitaifa kumechangia Azimio kukosa makali ya kuhakiki serikali ya Rais William Ruto.
“Mbali na hayo, vinara wengine wa Azimio kama vile aliyekuwa mgombea urais Raila Odinga, aliyekuwa mgombea mwenza Martha Karua na aliyekuwa Waziri Mkuu mtarajiwa Kalonzo Musyoka wamechelea kutoa taarifa za pamoja kuhusu masuala ya kitaifa. Hali hii imetoa picha ya uwepo wa mgawanyiko katika upinzani,” asema Bw Martin Andati ambaye ni mchanganuzi wa masuala ya kisiasa.
Alikuwa akirejelea taarifa ambayo Bw Odinga alitoa Alhamisi kuhusu visa vya utovu wa usalama, ukiukaji wa sheria na kuporomoka kwa kesi ya ufisadi ya Sh7.4 iliyomkabili Naibu Rais Rigathi Gachagua. Kwa upande mwingine, Bw Musyoka alikuwa katika kaunti ya Machakos alikokashifu mpango wa serikali wa kuwafurusha maskwota wanaodaiwa kuishi katika ardhi ya kampuni moja ya saruji eneo la Mavoko kinyume cha sheria.
“Vinara wa Azimio walipaswa kutoa taarifa za pamoja kuhusu masuala haya kudhihirisha umoja kati yao, ambayo yanaweza kutikisa serikali ya Dkt Ruto na kuilazimisha kokomesha vitendo vinavyoonekana kwenda kinyume na msingi wa uongozi bora,” Bw Andati akasema.
Tishio la wabunge wa Jubilee kwamba watagura Azimio kutokana na kile wanachodai ni kutotendewa haki katika ugavi wa nyadhifa katika asasi muhimu za bunge pia linadhihirisha hali ya utovu wa uongozi thabiti katika muungano huo.
Mnamo Alhamisi, wabunge hao walisema hawataendelea kushirikiana na wenzao wa vyama vya ODM na Wiper ikiwa mmoja wao hataruhusiwa kupewa nafasi ya kuwa mwanachama wa Tume ya Huduma za Bunge (PSC).
Wakiongozwa na naibu kiranja wa wachache Sabina Chege wabunge hao walikerwa na hatua ya kuondolewa kwa jina la kiranja wa wachache katika seneti Fatuma Dullo kwenye orodha ya wawakilishi wa Azimio na nafasi yake kupewa Seneta wa Nyamira, Okong’o Omogeni (ODM).
Jubilee
“Nafasi ya Seneta Dullo ilifaa kuchukuliwa na mwanachama wa Jubilee wala si ODM. Hii ni kwa sababu Jubilee ni mojawapo ya vyama vikubwa katika muungano wa Azimio, baada ya ODM na Wiper,” Bi Chege akawaambia wanahabari katika majengo ya bunge, Nairobi.
“Isitoshe, uongozi wa Azimio pia haujatutendea haki kisiasa kama Jubilee wakati wa ugavi wa nafasi za uanachama na uongozi katika kamati za bunge la kitaifa na Seneti. Hii sio haki na hatutaendelea kukaa katika uhusiano kama huu,” akaongeza Bi Chege, ambaye ni mbunge maalum.
Kwa upande wake, mbunge wa Eldas, Aden Keynan alisema chama cha Jubilee kitaandaa mkutano wa kundi la wabunge wake (PG) kujadili mustakabali wao ndani na nje ya bunge kuanzia sasa hadi uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2027.
Chama cha Jubilee kina jumla ya wabunge 26 katika bunge la kitaifa na hivyo kujiondoa kwake kutoka muungano wa Azimio kutadhoofisha zaidi mrengo huo bungeni.
Mchangnuzi wa masuala ya kisiasa Javas Bigambo anasema ni kinaya kwamba chama cha Jubilee kinatisha kujiondoa kutoka Azimio ilhali, Bw Kenyatta, ambaye ni kiongozi wake, ndiye kiongozi wa baraza kuu la muungano huo.
“Hali hii inaashiria utovu wa uongozi na mshikamano katika muungano huu ambao una wajibu wa kuhakiki utendakazi wa serikali kuu kwa manufaa ya Wakenya,” anasema.
Kulingana na Bw Bigambo uongozi wa Azimio unafaa kufanya mikutano ya kila mara na wawakilishi wao katika Bunge la Kitaifa na Seneti ili kuwapa mwelekeo wa namna ya kukabiliana na nrengo tawala, Kenya Kwanza.
“Hata ingawa Bw Kenyatta alipewa wajibu wa Balozi Maalum wa Kenya kuhusu Shughuli za kuleta Amani nchini Ethiopia na ukanda wa Afrika Mashariki, atenge muda wa kupalilia umoja na uthabiti katika muungano wa Azimio. Hii ni kwa sababu, ilivyo sasa, yeye ndiye mwenyekiti wa baraza kuu la Azimio,” anaongeza.
Subscribe our newsletter to stay updated