NA SAMMY WAWERU
MHUDUMU wa bucha eneo la Ruiru, Kiambu anaandamwa na mkono wa sheria baada ya kutumbukiza kijana kwenye sufuria ya supu inayochemka.
Mvulana huyo anayekisiwa kuwa chini ya umri wa miaka 20, inasemekana husambaza mifuko ya kupakia bidhaa kwa kutumia pikipiki.
Kulingana na walioshuhudia, alikuwa ameegesha pikipiki karibu na alikokuwa akipikia supu mshukiwa.
“Alikuwa katika harakati za kusambaza bidhaa anazochuuza,” akasema Grace Njeri, mmoja wa walioshuhudia.
Tukio hilo lilifanyika wikendi katika eneo la Kwa Kairu, Ruiru.
Inaarifiwa kwamba wawili hao walianza kurushiana maneno, mhudumu wa bucha akitaka mfanyabiashara huyo mchanga kuondoa pikipiki yake haraka iwezekanavyo.
Licha ya kijana huyo kumrai ampe muda mfupi, majibizano kati yao yaliishia jamaa kumnyanyua na kumtumbukiza kwenye sufuria kubwa iliyokuwa ikitokota supu.
Mwathiriwa aliuguza majeraha mabaya, walioshuhudia na wapitanjia wakitishia kutia adabu mwanabucha huyo.
Alijifungia kwenye mojawapo ya maduka ili kuokoa maisha yake.
Umma uliokuwa na ghadhabu nusra uvunje mlango wa duka hilo, ukiapa kumwadhibu.
“Huyu kijana ni sawa na mtoto wake. Ni unyama ulioje kumtendea ukatili wa aina hii kwa kumchoma kwa supu?” Ken Kamau mhudumu wa bodaboda eneo la Kwa Kairu alishangaa.
Mshukiwa aliokolewa na chifu eneo hilo, aliyerai watu kutochukua sheria mikononi mwao.
Hata licha ya mvulana huyo kuuguza majeraha mabaya, mamake alipofika alishangaza akidai hatamchukulia hatua kisheria ila Mungu atamwadhibu.
“Nimemwachia Mungu, atanilipizia kisasi,” mama huyo aliyelemewa na machozi alisema.
Taifa Leo Dijitali imebaini kuwa mhudumu huyo wa bucha amekuwa na visa kadhaa vya kuvamia watu hasa anaotofautiana nao.
“Si mara ya kwanza kuzua vita. Amekuwa na mazoea ya kupiga watu, hata wateja wake,” alisema mkazi aliyeomba kubana majina yake.
Cha kushangaza ni kwamba anaposhtakiwa kwa maafisa wa usalama, hakuna hatua inayochukuliwa.