NA FRIDAH OKACHI
MFANYABIASHARA Jamal Marlow almaarufu Jamal Rohosafi kwa mara ya kwanza amezungumza baada ya kufanyiwa upasuaji wa kupandikiziwa nywele kwenye kichwa chake mara ya pili.
Jamal alichapisha video na picha za kupandikiziwa nywele kwenye kichwa nchini Uturuki.
Tatizo la kukosa nywele miongoni mwa wanaume na wanawake limekuwa likiwakabili wengi. Baadhi ya wanaume na wanawake wamekuwa wakihisi hawako sawa kutokana na nywele chache walizo nazo.
Januari 2023, Jamal alienda nchini Uturuki kupandikiziwa nywele.
Kutokana na joto la malumbano kati ya Jamal na aliyekuwa mke wake Bira Amira suala la nywele liliibuliwa. Amira alichapisha picha ya Jamal na kuandika maneno yafuatayo, “… alienda Uturuki kufanyiwa upasuaji… nimlemavu… Ehe, nywele ni nini? Kwa nini ulifanyiwa upasuaji wa kupandikizwa nywele? ili kuinua hadhi yako?”
Mnamo Septemba 29, 2023, Jamal alichapisha picha zake wakati wa shughuli ya kupandikizwa nywele,akiwa katika hospitali ya Iconica International Clinic, nchini Uturuki.
“Daktari ambaye nafasi yake duniani ni bora kwenye maswala ya kupandikizwa nywele, hivi karibuni atakuwa Kenya na Afrika kote,” aliandika kwenye ukurasa wake wa Instagram
Kulingana na Jamal, watu wengi hapa nchini Kenya hawafahamu kuhusu kupandikizwa kwa nywele. Jamal alielezea mashabiki wake kuwa upasuaji wa kupandikizwa nywele huhusisha kutolewa sehemu nywele zipo nyingi na kuwekwa sehemu ambapo hakuna nywele.
Upasuaji wa kupandikiziwa nywele unaweza kugharimu Sh1 milioni.
“Yangu ilitolewa kutoka sehemu ya nyuma kwa kichwa changu na kupandikizwa mbele. Kwa siku chache sehemu ambapo walitoa nywele, itaota. Upasuaji huu si mchungu,” aliongezea.
Sehemu iliyopandikizwa nywele huota baada ya miezi kumi na miwili hadi miezi kumi na minane ili kuonekana.
Jamal ni kiongozi wa muungano wa matatu na mkurungezi mkuu wa Huduma Credit.