• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
‘Sauti ya Mnyonge’ anayeendeleza ndoto ya kutetea maskini nchini akiwa Iceland

‘Sauti ya Mnyonge’ anayeendeleza ndoto ya kutetea maskini nchini akiwa Iceland

Na BENSON MATHEKA

ALILAZIMIKA kuondoka Kenya akidai kwamba maisha yake yalikuwa hatarini kwa sababu ya kutetea haki za maskini.

Alikuwa amejitolea kuzuia ardhi ya maskini kunyakuliwa na watu walio na ushawishi, baadhi yao mabwenyewe na maafisa wa serikali. Katika eneobunge la Othaya, Kaunti ya Nyeri alikozaliwa, anafahamika kama “Sauti ya Mnyonge” kwa sababu ya kutetea haki za akina yakhe.

Na japo alitorokea Iceland, anakoishi uhamishoni hadi wakati huu, David Kimengere Waititu, angali anaendeleza shughuli zake za uanaharakati nchini.

“Siwezi kunyamaza ndugu na dada zangu nchini Kenya wakiendelea kunyanyaswa na mabwanyenye na wanasiasa. Nitaendelea kufanya kila niwezalo kuhakikisha haki zao zinaheshimiwa kupitia utawala bora, uwazi na uwajibikaji,” Kimengere aliambia Taifa Leo kwa simu kutoka Iceland.

Akiwa uhamishoni, amekuwa akifuatilia kwa makini yanayotendeka nchini na kutumia mitandao kuhimiza Wakenya wasivunjike moyo bali waungane kutetea na kulinda haki zao.

“Nimeanzisha na kusajili shirika kwa jina ‘Kuunga, Kujenga Kenya’ kwa lengo ya kuunganisha akina yakhe wazungumze kwa sauti moja. Hii ni baada ya kugundua kwamba wanasiasa wamekuwa wakiwagawanya kwa misingi ya kikabila ili wasiwe na nguvu za kutetea haki zao,” asema Kimengere.

Hata hivyo, alikataa kufichua majina ya anaoshirikiana nao nchini kwa usalama wao. Kimengere 48, ambaye ni mzaliwa wa kijiji cha Kihome, Othaya Kaunti ya Nyeri, alianza shughuli za uanaharakati akiwa mchuuzi mjini Nyeri.

Alijiunga na siasa ili kupata nafasi ya kutetea haki za maskini kwa kugombea kiti cha ubunge cha Othaya lakini hakufua dafu. Kwenye uchaguzi mkuu wa 2013, alikamatwa kwa madai ya kukiuka kanuni za uchaguzi, hatua ambayo anasema ilichochewa na wapinzani wake waliohisi kwamba akiwa mtoto wa maskini, hakufaa kushindana nao.

Kimengere anasema kwamba maskini nchini wanateseka kwa sababu hawapati nafasi za uongozi zinazochukuliwa kuwa za watu wa tabaka la juu.

“Maskini nchini Kenya wanachukuliwa kama watumwa wa wanasiasa na mimi nimejitolea kujaza pengo kwa kuwaunganisha wafungue macho. Kenya si ya familia chache zinazopora pesa za umma na kuzitumia kwa kampeni za uchaguzi mkuu,” asema.Mwanaharakati huyu anasema aliondoka nchini baada ya kutishiwa maisha na watu wenye ushawishi alipowasilisha kesi kadhaa kupinga juhudi zao za kunyakua ardhi ya maskini.“Sitataja watu hao kwa kuwa kesi zingali kortini,” asema.

“Nililazimika kuacha familia yangu Kenya nilipopashwa habari kwamba kulikuwa na njama ya kunidhuru kwa sababu watu fulani hawakufurahia juhudi zangu za kuhakikisha maskini wanapata haki yao,” asema baba huyo wa watoto watatu.

Mbali na kupiga vita unyakuzi wa ardhi, Kimengere pia anahakikisha kuwa raia wanaelewa haki zao kama wapigakura ili waweze kufanya maamuzi ya busara wakati wa uchaguzi.Hii ndiyo sababu aliungana na Wakenya wengine kusajili shirika la Commonwealth Voters Privileges Rights Association ( COWE-VOPRA) ambalo wamekuwa wakitumia kuhamasisha raia kuhusu haki zao.

“Kuna pengo kubwa kwa sababu wanasiasa wakuu hawataki maskini wajue haki zao. Hii ndio sababu elimu ya jamii kuhusu uchaguzi haitekelezwi ipaswavyo kabla ya uchaguzi mkuu na ikifanyika huwa inalenga kuwagawanya Wakenya na kuwafanya wapigane,” asema.

Anatoa mfano wa mchakato wa kubadilisha katiba kupitia mpango wa maridhiano ambao anasema umegawanya Wakenya kwa misingi ya kimaeneo na kijamii japo ulidaiwa kuwa wa kuwaunganisha.

“Kwa kuwa ulikuwa na nia fiche, uliendeshwa kiholela licha ya mashirika ya kijamii kusisitiza raia walifaa kupatiwa nakala wajisomee na kuuelewa kabla ya kuupigia kura,” alisema.

Kupitia Cowe-vopra, Kimengere alipinga mchakato huo ulipoasisiwa na kuandikia kamati ya watu 14 iliyosimamiwa na aliyekuwa Seneta wa Garissa, Yusuf Haji kutaka usitishwe.

“Sisi katika Cowe-vopra tuliona mbele. Tuling’amua kwamba mchakato huo ulikuwa wa kupumbaza raia hasa maoni ya makundi mbali mbali ya kijamii na kidini yalipopuuzwa na tukaandikia kamati ya Haji iusitishe,” aeleza.

Barua yao ilipokelewa na maspika wa bunge ambao pia hawakuwa na uwezo kwa kuwa mswada huo haukuwa umewasilishwa kwao.Kimengere anasema kwamba hakuna kitakachomzuia akome kutetea haki za maskini.

“Mimi ni hasla wa kweli. Ninajua uchungu na mateso ya akina yakhe na ninahisi nikiungana na wenzangu ambao wanajali nchi yao bila tamaa, siku moja tutabadilisha mwelekeo wa demokrasia ya Kenya,” asema.

Anakanusha madai kwamba alienda Iceland kutafuta pesa za kufadhili shughuli zake za uanaharakati akisema mashirika mawili anayofanya kazi nayo hayana ufadhili wowote kutoka nje ya nchi.

“Nilikuja Iceland kama mkimbizi kuokoa maisha yangu na si kuja kutafuta misaada. Ni mkimbizi gani aliye na uhuru wa kutembelea ofisi za mashirika kuomba pesa za kuendeleza uanaharakati katika nchi aliyoacha wazazi na jamaa zake anaowapenda?” anahoji.

Katika eneobunge la Othaya, anafahamika kama “Sauti ya Mnyonge Roho Safi “ kwa sababu ya kujitolea kwake kutetea haki za maskini.

“Kimengere ni mtu wa roho safi sana na hataki kuona mtu akidhulumiwa,” asema James Kamuiru, mhudumu wa matatu mjini Othaya.“Ninajua siku moja Kenya itakuwa nchi ya haki kwa raia wake wote. Mungu anaipenda Kenya na hataiacha iangamizwe na utawala mbaya,” asema.

You can share this post!

Ukeketeji Mlima Kenya unavyochochewa na laana

BBI YAINGIA ICU