KWA HISANI YA KENYA YEAR BOOK
NJENGA Karume na Mwai Kibaki walikuwa marafiki wa dhati. Lakini jinsi Karume aliyeacha masomo akiwa darasa la nne aliweza kuwa rafiki mkubwa wa mwanauchumi, ambaye hakuwa amefunza katika Chuo Kikuu cha Makerere pekee lakini aliyekuwa amepita mitihani yake kwa alama za juu katika Makerere na Chuo Kikuu cha Uchumi cha London ndiyo ilikuwa alama ya urafiki wao.
Mnamo Juni 2004, wakati Kibaki alikumbwa na uasi katika serikali yake, alimwendea Karume aliyekuwa mbunge wa chama cha Kanu, kujiunga na Baraza la Mawaziri la muungano tawala wa National Rainbow Coalition (NARC) chini ya serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Walikuwa wamekutana katika Ikulu ya Nairobi baada ya Karume kuitwa na Mkuu wa Utumishi wa Umma na Katibu wa Baraza la Mawaziri Francis Muthaura, kutoka Mombasa.
“Nilishangaa sana” alisema baadaye.
“Ilikuwa imeshukiwa kwamba Kibaki angemteua Paul Muite ili kuwa na mbunge kutoka Kiambu katika baraza lake la Mawaziri.”
Lakini Karume alikuwa amechaguliwa kujiunga na baraza la mawaziri lililojumuisha Simeon Nyachae wa FORD-People, John Koech na William ole Ntimama wa Kanu katika juhudi za kuwa na usawa wa kimaeneo kujumuisha hata maeneo ambayo hayakuwa yamepigia kura NARC kwenye uchaguzi mkuu wa Desemba 2002.
Karume aliteuliwa kusimamia wizara mpya iliyobuniwa ya Mpango Maalumu.
Wakati huo, Kenya ilikuwa ikikumbwa na hali mbaya ya uchumi na jukumu la kwanza la Karume lilikuwa ni kushirikiana na mashirika ya kibinadamu na idara za serikali kupata chakula na maji kwa jamii zilizoathiriwa. Karume alizaliwa mwaka wa 1929 katika eneo la Elmentaita, Rift Valley, ambako familia yake ilikuwa imehamia kutoka Kiambu.
Aliacha shule akiwa na umri mdogo na alikuwa na bahati kujiunga na Jean School Kabete, na baadaye Kenya Institute of Administration (Sasa Kenya School of Government), alipopata cheti katika masomo ya biashara.
Alianza kufanya biashara akiwa na umri mdogo kwa kuuza makaa, mbao na ngozi kabla ya kujiunga na biashara ya pombe.
Ni akiwa kiongozi wa chama cha jamii za Gikuyu Embu na Meru (GEMA) ambapo aliibuka kuwa mmoja wa waliokuwa na ushawishi katika utawala wa Rais Jomo Kenyatta.
GEMA ilikuwa imeundwa 1971 kama shirika la kijamii; baadaye Karume alikuwa sura ya shirika hilo. Lakini Gema ilichukiwa na baadhi ya washauri wa Rais Jomo Kenyatta akiwemo Mkuu wa Sheria (AG) Charles Njonjo.
Maafisa wake wa muda walikuwa Gikonyo Kiano (mwenyekiti), Lucas Kamau (katibu mkuu), Kibaki (Mweka hazina ) na Waruru Kanja (katibu mtendaji). Mwaka wa 1973 Karume alichaguliwa mwenyekiti. Kibaki hakutetea kiti chake na Jacob M’mwongo alichaguliwa mweka hazina.
Baadaye Karume alidai kwamba uamuzi wa Kibaki wa kuondoka Nairobi alikokuwa mbunge wa Donholm kugombea kiti cha ubunge cha Othaya kulitokana na presha kutoka GEMA.
Baada ya miezi michache katika wizara ya Mipango Maalum, Kibaki alimhamisha hadi wizara ya Ulinzi.
Akiwa waziri, Karume alisalia mmoja wa wandani ambao Kibaki aliamini zaidi.
Subscribe our newsletter to stay updated