NA CECIL ODONGO
WANASIASA kutoka eneo la Luo Nyanza ambao wamehamia upande wa serikali wanastahili kuheshimu kinara wa ODM, Raila Odinga na jamii hiyo ambayo bado ina makovu baada ya kigogo wao kushindwa kwenye uchaguzi mkuu uliopita.
Wakati wa ziara ya Waziri wa Teknolojia na Mawasiliano Eliud Owalo ya kusambaza chakula katika kaunti za Luo Nyanza wikendi iliyopita, baadhi ya wanasiasa ambao waliandamana naye walitumia majukwaa waliyopewa kukejeli siasa za waziri huyo mkuu wa zamani na kuzihusisha na umaskini wa jamii hiyo.
Japo waziri alikuwa muungwana na hakuzungumzia siasa, wengine walioandamana naye walienda hatua zaidi na kuanza kuiharakisha jamii hiyo kuondoka upinzani ili ijiunge na Kenya Kwanza.
Wanasiasa hawa wanastahili kutambua kuwa, bado wengi wana makovu baada ya Raila kupoteza kura na wanastahili kuachwa waugue taratibu badala ya kuharakishwa kuiunga serikali.
Pili, katika utamaduni wa Waluo na hata kwingineko Afrika, mtu anapokusaidia kwa kukupa chakula, huwa hafanyi hivyo kwa masharti wala hakudhalilishi kwa sababu wema huo ni ishara ya utu.
Ni aibu kuwa wanasiasa hawa walitumia jukwaa la kuwapa watu chakula cha msaada kuikejeli jamii kwa kupoteza kura na hata kuwaambia watapata ‘mazuri’ zaidi wakiunga utawala wa Kenya Kwanza.
Kinaya ni kuwa, wanasiasa waliokuwa wakiropokwa katika mikutano hiyo ni wale ambao siasa zao zilijengeka enzi walipokuwa ODM na hata waliwahi kuchaguliwa kwenye ubunge, ugavana, useneta, uwaziri na hata katika mashirika ya serikali kutokana na hisani ya waziri huyo mkuu wa zamani.
Subscribe our newsletter to stay updated