MNAMO Aprili mwaka 2021, Shirika la Huduma za Jiji la Nairobi lilianzisha mradi wa uboreshaji wa masoko manane ya wazi jijini Nairobi.
Mradi huo ulihusisha ujenzi wa vibanda vya kisasa vya kufanyia biashara, maeneo ya kuegesha magari, vyoo vya kisasa na barabara ndogo za kuelekea katika masoko hayo.
Miongoni mwa masoko yaliyolengwa kuboreshwa katika mradi huo ni pamoja na Soko la Muthurwa, Soko la City Park, Soko la Jericho, Soko la Wakulima, Soko la Toi lililoko mtaa wa Kibera, miongoni mwa masoko mengine.
Mkurugenzi wa NMS Luteni Jenerali Mohamed Badi alitangaza kuwa mradi huo ulilenga kupanua nafasi za biashara kwa wakazi wa Nairobi, ambazo, awali, zilikuwa finyu.
Lakini safu hii inamkumbusha Luteni Badi kuwa masoko matatu katika maeneo ya Mwariru, Westland na Karandini ambayo yaligharimu Sh2.2 bilioni, yalikamilishwa Oktoba, 2021 lakini mpaka sasa hayajazinduliwa rasmi.
NMS inafaa izindue masoko haya kabla ya uchaguzi mkuu wa Agosti 9 ili wafanyabiashara wapate nafasi ya kuendeshea biashara.