Na GEOFFREY ANENE
MADEREVA 20 wanatarajiwa kuwania ubingwa wa duru ya nane ya Mbio za Magari za Kitaifa za Kenya (KNRC) KCB Thika Rally mnamo Novemba 20-21.
Bingwa wa Afrika Carl “Flash” Tundo (Mitsubishi Evo 10), Baldev Chager (Volkswagen Polo) na Karan Patel (Ford Fiesta) ni baadhi ya majina makubwa yatakayoshiriki mbio hizo za kilomita 142.18.
Makinda McRae Kimathi (Ford Fiesta) na Hamza Anwar (Mitsubishi Evo 10) na dereva mwanamke pekee Maxime Wahome (Subaru Impreza) pia wako kwenye orodha ya washiriki wa mbio hizo zitakazoanzia katika Chuo Kikuu cha Mount Kenya na kukamilika mle baada ya kufanya mikondo ya Buffalo, Ananas, Pavillion na Ndula.
Kinda matata Jeremy Wahome pamoja na jagina Ian Duncan ni baadhi ya madereva watakaokosekana katika duru hiyo inayoweza kushuhudia Tundo akitawazwa bingwa wa Kenya akitwaa taji ikiwa ataibuka mshindi naye Chager ateleze tena.
Alitawala duru ya KCB Nanyuki mnamo Oktoba 9.
Chager, ambaye alishinda taji la kitaifa mara ya mwisho KNRC ilifanyika mwaka 2019, alimaliza nambari 10 mjini Nanyuki.