Na MASHIRIKA
BARCELONA waliendelea kutamba katika Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) msimu huu wa 2022-23 kwa kukung’uta Girona 1-0 ugani Montilivi.
Miamba hao wanawania ufalme wa La Liga kwa mara ya kwanza tangu 2018-19.
Bao la pekee katika pambano lao dhidi ya Girona lilijazwa kimiani na chipukizi Pedri Lopez aliyekuwa akinogesha mchuano wake wa 100 katika mashindano yote akivalia jezi za Barcelona.
Chini ya kocha Xavi Hernandez, Barcelona sasa hawajashindwa katika mechi 13 zilizopita katika mashindano yote. Wameshinda mechi nane na kupiga sare moja ligini tangu Real Madrid wawapokeze kichapo cha 3-1 ugani Bernabeu mnamo Oktoba 2022.
Matokeo hayo yanawadumisha kileleni mwa jedwali kwa alama 47 kutokana na michuano 18. Sawa na Sevilla waliopepeta Elche 3-0, Girona pia wamejizolea pointi 21 kutokana na mechi 19.
Kocha wa Girona, Michel Munoz, alionyeshwa kadi nyekundu wakati wa mechi yao dhidi ya Barcelona kwa utovu wa nidhamu alipolalamikia tukio la mwanasoka wake, Rodrigo Riquelme, kuchezewa visivyo na Frenkie de Jong.
Barcelona waliokosa huduma za washambuliaji Robert Lewandowski na Ferran Torres walisalia butu katika safu ya uvamizi baada ya fowadi Ousmane Dembele kuondolewa ugani katika kipindi cha kwanza kutokana na jeraha la paja.
MATOKEO YA LA LIGA:
Girona 0-1 Barcelona
Cadiz 2-0 Mallorca
Sevilla 3-0 Elche
Getafe 0-1 Real Betis
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO