Na MASHIRIKA
BARCELONA walifungua pengo la pointi 11 kileleni mwa jedwali la Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) baada ya kusajili ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Villarreal mnamo Jumapili ugani De la Ceramica.
Bao la pekee katika mchuano huo lilipachikwa wavuni na Pedri Gonzalez Lopez katika dakika ya 18. Ushindi huo ulikuwa wa sita mfululizo msimu huu kusajiliwa na mabingwa hao mara 26 wa La Liga.
Chini ya kocha Xavi Hernandez, Barcelona kwa sasa wamefungwa mabao saba pekee ligini na kichapo cha pekee walichopokea katika La Liga ni dhidi ya mabingwa watetezi Real Madrid mnamo Disemba 2022.
Barcelona sasa wana alama 56 huku pengo la pointi 11 likitamalaki kati yao na nambari mbili Real waliotawazwa wafalme wa Klabu Bingwa Duniani mnamo Februari 11, 2023 baada ya kupepeta Al-Hilal ya Saudi Arabia 5-3.
Real watarejelea kampeni za La Liga mnamo Februari 15, 2023 dhidi ya Elche uwanjani Bernabeu. Villarreal kwa sasa wanakamata nafasi ya nane kwa alama 31, saba nyuma ya nambari nne Atletico Madrid.
MATOKEO YA LA LIGA (Jumapili):
Villarreal 0-1 Barcelona
Getafe 1-1 Rayo Vallecano
Celta Vigo 0-1 Atletico Madrid
Real Valladolid 0-0 Osasuna
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO