Na MASHIRIKA
NYOTA wa zamani wa Chelsea, Gonzalo Higuain, 34, atastaafu soka mwishoni mwa msimu huu wa 2021-22.
Makali ya sogora huyo raia wa Argentina yameshuka pakubwa tangu aagane na Juventus na kuyoyomea Amerika mnamo 2020 kuvalia jezi za Inter Miami katika Major League Soccer (MLS).
Chini ya kocha Phil Neville, Inter Miami hawajashinda mechi yoyote kati ya tano za ufunguzi wa msimu huu wa MLS.
Mkataba wa Higuain na miamba hao unatarajiwa kutamatika rasmi mnamo Disemba 2022 na sogora huyo hatakuwa radhi kurefusha zaidi kandarasi hiyo wala kuelekea kwingine kwa ajili ya kusakata soka ya kulipwa.
Jorge ambaye ni baba na wakala wa Higuain amefichua kwamba huenda sogora huyo akajitosa katika ulingo wa ukufunzi wa soka.
Tangu akose kuridhisha kwenye fainali za Kombe la Dunia mnamo 2014 nchini Brazil, makali ya Higuain yamekuwa yakishuka pia katika kiwango cha soka ya kitaifa huku akishindwa kuongoza Argentina kuzoa taji la Copa America mnamo 2015 na 2016.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO