• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 9:11 AM
Jamhuri ya Czech yaduwaza Uholanzi na kujikatia tiketi ya kumenyana na Denmark kwenye robo-fainali za Euro

Jamhuri ya Czech yaduwaza Uholanzi na kujikatia tiketi ya kumenyana na Denmark kwenye robo-fainali za Euro

Na MASHIRIKA

JAMHURI ya Czech waliduwaza mashabiki katika uwanja wa Puskas Arena nchini Hungary mnamo Jumapili baada ya kuwapokeza Uholanzi kichapo cha 2-0 kilichowaondoa kwenye hatua ya 16-bora ya Euro.

Ushindi wa Czech ulichangiwa pakubwa na tukio la Uholanzi kusalia ugani na wachezaji 10 pekee baada ya beki Matthijs de Ligt wa Juventus kuonyeshwa kadi nyekundu katika dakika ya 55.

De Ligt ambaye ni mchezaji wa zamani wa Ajax, aliunawa mpira ambao vinginevyo ungejazwa kimiani na fowadi matata wa Czech, Patrik Schick.

Tomas Holes aliwafungulia Czech ukurasa wa mabao kunako dakika ya 68 kabla ya kuchangia jingine lililofumwa wavuni na Schick katika dakika ya 80.

Uholanzi waliokuwa wanafainali wa Uefa Nations League mnamo 2019, walianza mechi kwa matao ya juu huku Donyell Malen akipoteza nafasi ya wazi ya kuwaweka kifua mbele baada ya kusalia peke yake na kipa Tomas Vaclik katika dakika ya nane.

Hata hivyo, ni Czech ambao wanashikilia nafasi ya 40 duniani, ndio walinyamazisha wapinzani wao wanaoorodheshwa wa 16 kimataifa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

Ushindi huo wa Czech uliwakatia tiketi ya kuvaana na Denmark kwenye hatua ya nane-bora mnamo Julai 3, 2021 nchini Azerbaijan. Denmark waliopigwa na Czech 3-0 kwenye robo-fainali za Euro mnamo 2004, waliingia hatua ya nane-bora mwaka huu mnamo Juni 26 baada ya kuwaponda Wales 4-0 jijini Amsterdam, Uholanzi.

Mbali na Malen, wanasoka wengine wa Uholanzi ambao walipoteza nafasi za kufunga mabao ya kurejesha kikosi chao mchezoni ni Denzel Dumfries, Patrick van Aanholt na Memphis Depay ambaye ni sajili mpya wa Barcelona.

Schick kwa sasa anajivunia mabao manne, moja pekee nyuma ya Cristiano Ronaldo ambaye alishuhudia kikosi chake cha Ureno kikibanduliwa na Ubelgiji mnamo Juni 27. Schick ni miongoni mwa wanasoka wanaopigiwa upatu wa kutwaa kiatu cha dhahabu kwenye kipute cha Euro mwaka huu.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Shujaa na Lionesses watiwa katika makundi ya kifo ya...

Familia ya Alvaro Morata yatishiwa maisha baada ya kupoteza...