• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 6:39 PM
Kane afunga mabao matatu na kuongoza Uingereza kuponda Albania

Kane afunga mabao matatu na kuongoza Uingereza kuponda Albania

Na MASHIRIKA

UINGEREZA sasa wanahitaji alama moja pekee kutokana na mchuano wa mwisho wa Kundi I dhidi ya San Marino ugenini mnamo Novemba 15, 2021 ili kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za 2022 nchini Qatar.

Hii ni baada ya kikosi hicho cha kocha Gareth Southgate kupepeta Albania 5-0 mnamo Ijumaa usiku ugani Wembley, Uingereza. Harry Kane aliongoza Uingereza kusajili ushindi huo mnono kwa kupachika wavuni mabao matatu katika kipindi cha kwanza.

Mabao mengine ya Uingereza yalifumwa wavuni katika kipindi cha kwanza kupitia Harry Maguire na Jordan Henderson baada ya wawili hao kushirikiana vilivyo na Reece James na Phil Foden. Kane kwa sasa ameifikia rekodi ya nguli Jimmy Greaves aliyewahi kufungia Uingereza mabao 44.

Nyota huyo wa Tottenham Hotspur amepachika wavuni mabao 39 kutokana na mechi za ushindani akivalia jezi za Uingereza, ufanisi ambao umemwezesha kuvunja rekodi ya Wayne Rooney aliyetikisa nyavu za wapinzani mara 37. Mamuzi ya kocha Southgate kuwajibisha viungo wawili wakabaji – Henderson na Kalvin Philips yalitiliwa shaka na mashabiki na wachanganuzi wa soka awali. Mfumo wake huo ulikuwa sawa na ule ulioshuhudia Uingereza wakikomoa Ujerumani kwenye kampeni za Euro 2020 kabla ya mfumo huo kuwaponza walipokutana na Italia kwenye fainali ya kipute hicho mnamo Julai 11, 2021 ugani Wembley.

Uingereza walitegemea James na Ben Chilwell kuwa mabeki wa kupanda na kushuka dhidi ya Albania huku Henderson akiachiwa nafasi kubwa ya kusuka mashambulizi.

Ingawa Maguire alisherehekea bao lake kwa kushika kutia vidole masikioni ili kuashiria kwamba amenyamazisha wakosoaji wake, wachanganuzi wa soka wanahisi kwamba itachukua muda zaidi kabla ya kumbukumbu za kudhalilishwa kwa Manchester United katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) katika siku za hivi karibuni kufutika.

Masihara ya Maguire katika safu ya ulinzi ya Man-United yalishuhudia mabingwa hao mara 20 wa EPL wakipondwa 5-0 na Liverpool kabla ya Man-City kuwatandika 2-0 ugani Old Trafford.

Mechi dhidi ya Albania ilimpa Southgate jukwaa mwafaka la kumwajibisha kiungo wa Arsenal, Emile Smith Rowe kwa mara ya kwanza ndani ya timu ya taifa.

You can share this post!

Mshindi wa Kundi C kati ya Italia na Uswisi kuamuliwa na...

Poland wazamisha Andorra kirahisi katika gozi la Kundi I

T L