• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
Kenya Lionesses wazidiwa maarifa na New Zealand raga ya akina dada ikianza Olimpiki

Kenya Lionesses wazidiwa maarifa na New Zealand raga ya akina dada ikianza Olimpiki

Na GEOFFREY ANENE

KENYA Lionesses wameanza kampeni yao ya pili kwenye Olimpiki kwa kuzabwa 29-7 na miamba New Zealand katika makala ya 2020 jijini Tokyo, Japan mnamo Julai 29.

Katika mechi hiyo ya Kundi A, Lionesses ya kocha Felix Oloo ilijipata chini alama 17-0 baada ya mabingwa hao wa Raga za Dunia kufunga miguso miwili kupitia kwa Michaela Blyde na mguso mmoja kutoka kwa Portia Woodman pamoja na mkwaju mmoja kupitia kwa Tyla Nathan-Wong.

Kenya ilipunguza mwanya huo hadi 17-7 kabla ya mapumziko baada ya kupachika mguso kupitia kwa Christabel Lindo ulioandamana na mkwaju wake.

Hata hivyo, matumaini ya Kenya kujifufua zaidi yalizimwa wakati New Zealand maarufu kama Black Ferns iliongeza miguso miwili katika kipindi cha pili kutoka kwa Stacey Fluher na Gayle Broughton pamoja na mkwaju kutoka kwa Nathan-Wong.

Kenya, ambayo ilijikatia tiketi ya Olimpiki za Tokyo baada ya mabingwa wa Afrika Kusini kujiondoa, itamenyana na Urusi katika mechi yake ijayo hapo saa saba mchana leo Alhamisi.

Kitakuwa kibarua kigumu dhidi ya Urusi ambayo ilipepeta Lionesses 41-0 wikendi ya Februari 20 na 17-5 wikendi ya Februari 27-28 katika mashindano ya kupasha misuli moto jijini Madrid, Uhispania.

You can share this post!

Kaunti yakarabati barabara mbovu ingawa maarufu

Fiji wahifadhi nishani ya dhahabu kwenye raga ya Olimpiki