• Nairobi
  • Last Updated May 21st, 2024 8:55 PM
Mashabiki wazomea Neymar na Messi kwa kutotambisha PSG katika UEFA

Mashabiki wazomea Neymar na Messi kwa kutotambisha PSG katika UEFA

Na MASHIRIKA

MASHABIKI wa Paris Saint-Germain (PSG) waliwazomea wachezaji wa kikosi hicho licha ya miamba hao kuwatandika Bordeaux 3-0 katika Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1).

Neymar na Lionel Messi walikuwa miongoni mwa wachezaji waliorushiwa cheche za matusi na mashabiki kutokana na tukio la PSG kudenguliwa na Real Madrid kwenye hatua ya 16-bora ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Machi 9, 2022.

Kylian Mbappe aliwafungulia PSG ukurasa wa mabao ugani Parc des Princes kabla ya Neymar na Leandro Paredes kuongeza mengine na kusaidia waajiri wao kufungua mwanya wa alama 15 kati yao na nambari mbili Nice kileleni mwa jedwali la Ligue 1.

Chini ya kocha Mauricio Pochettino, wanasoka wa PSG walionyeshwa mapokezi baridi na mashabiki wao huku baadhi wakiimba nyimbo za kumshinikiza rais wa klabu Nasser Al-Khelaifi na mkurugenzi wa soka Leonardo Araujo kujiuzulu.

Ilivyo, taji la pekee ambalo Pochettino anaweza kushindia PSG muhula huu ni la Ligue 1 baada ya waajiri wake kudenguliwa pia kwenye French Cup.

Luis Suarez na Cesc Fabregas waliowahi kucheza pamoja na Neymar na Messi kambini mwa Barcelona ni miongoni mwa wanasoka ambao walitumia mitandao yao ya kijamii kurai mashabiki wa PSG kulegeza msimamo wao dhidi ya washambuliaji hao matata.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Arsenal wacharaza Leicester na kurejea ndani ya mduara wa...

Zain Manji aibuka mshindi wa Muthaiga Safaricom Golf Tour

T L