NA TOTO AREGE
NATION FC imejumuishwa katika Kundi C katika mashindano ya soka ya Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo (SJAK) yanayopigwa jeki na La Liga na yatakayofanyika Julai 1, 2023.
MediaMax FC, Makueni Journalists FC na Standard Media FC ndizo timu nyingine kwenye Kundi C.
Mashindano hayo ya siku moja, yatahusisha jumla ya timu 16 zitakazochuana katika kinyang’anyiro cha wachezaji watano kila upande katika jengo la Galleria Mall jijini Nairobi siku ya Jumamosi.
Timu hizo 16 zimepangwa katika makundi manne yenye timu nne kila moja. Kila mechi itachezwa kwa muda wa jumla ya dakika 12.
Ikiwa mechi itaishia sare katika muda wa kawaida, mechi itaelekea moja kwa moja kwenye awamu ya wachezaji kupiga mikwaju ya penalti.
Katika kila timu, lazima kuwe na mchezaji mwanamke wakati wowote wa mchezo na ikiwa timu itashindwa kufanya hivyo itapoteza mchezaji mmoja uwanjani.
Akizungumza katika uwanja wa Nyayo mnamo Jumanne wakati wa droo hiyo, mjumbe wa La Liga nchini Kenya Alvaro Abrev amesema mashindano hayo yatachangia pakubwa kuuza sera zao.
“Tumefurahishwa sana na ushirikiano na wanahabari. Mwaka 2024 tunataka kupeleka mashindano haya katika ngazi ya Afrika Mashariki. La Liga imefadhili programu za mashinani nchini Kenya na Tanzania na tunafurahi kwamba zote zimefanikiwa,” amesema Abrev.
Rais wa SJAK James Waindi amesisitiza haja ya timu hizo kufuata sheria zinazosimamia mashindano hayo.
“Imekuwa zaidi ya miaka mitano tangu tuwe na siku ya michezo na tunatarajia shughuli nyingi na furaha kubwa Jumamosi. Tulikuwa na timu 20 zilizoonyesha nia lakini tulipunguza hadi timu 16,” ameongeza Waindi.
Mshindi atatia mfukoni Sh50,000, mshindi wa pili atapokea Sh30,000 na timu itakayoshika nafasi ya tatu itarejea nyumbani na Sh20,000.
Kundi A
Cape Media group TV 47
Athletics News Fc
Royal Media services
Radio Africa Group
Kundi B
KBC FC
CGTN
Freelance Journalists
Supersport
Kundi C
MediaMax
Makueni Journalists
Nation FC
Standard Media FC
Kundi D
Kass FM
Coast Media FC
BBC
Mozzart bet Sports