• Nairobi
  • Last Updated May 20th, 2024 2:23 PM
Smalling aongoza AS Roma kutandika Spezia katika Serie A

Smalling aongoza AS Roma kutandika Spezia katika Serie A

Na MASHIRIKA

KOCHA Jose Mourinho aliongoza waajiri wake AS Roma kupepeta Spezia 2-0 katika Ligi Kuu ya Italia (Serie A) mnamo Jumatatu usiku.

Mechi hiyo ilikuwa ya kwanza kwa Roma kushinda kutokana na tatu ligini.

Chris Smalling aliwaweka Roma kifua mbele baada ya kushirikiana na Tammy Abraham katika dakika ya sita.

Abraham alishuhudia kombora lake likibusu mwamba wa goli la Spezia katika dakika ya 16 kabla ya Roger Ibanez kufanya mambo kuwa 2-0 katika dakika ya 56.

Matokeo hayo yalipaisha Roma hadi nafasi ya sita jedwalini kwa alama 28 sawa na Juventus wanaoshikilia nafasi ya saba. Roma walikamilisha mechi na wanasoka 10 pekee uwanjani baada ya Felix Afena-Gyan kuonyeshwa kadi ya pili ya manjano mwishoni mwa kipindi cha pili.

Hadi walipokomoa Spezia, Roma walikuwa wamepoteza mechi mbili mfululizo ligini dhidi ya Bologna na Inter Milan mwanzoni mwa mwezi huu.

Baada ya kutandaza jumla ya michuano 17, sasa ni pengo la alama 12 ndilo linatenganisha Roma na viongozi wa jedwali Inter Milan na wanajiandaa kumenyana na nambari tatu Atalanta mnamo Jumamosi.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

JIJUE DADA: Kuzuia ngozi kuzeeka mapema

Aubameyang apokonywa utepe wa unahodha kambini mwa Arsenal

T L