• Nairobi
  • Last Updated May 21st, 2024 7:05 PM
Southampton wamtimua kocha Nathan Jones

Southampton wamtimua kocha Nathan Jones

Na MASHIRIKA

SOUTHAMPTON wamemfuta kazi kocha Nathan Jones, 49, baada ya kuhudumu kambini mwao kwa siku 95 pekee.

Mkufunzi huyo wa zamani wa Luton Town anafurushwa ugani St Mary’s kikosi cha Southampton kikivuta mkia wa jedwali la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) kwa alama 15 pekee kutokana na mechi 22.

Kutimuliwa kwa Jones kulichochewa zaidi na matokeo duni yaliyoshuhudia Southampton wakipokezwa kichapo cha 2-1 na Wolverhampton katika EPL uwanjani St Mary’s.

Jones ambaye ni raia wa Wales, ndiye kocha ambaye amewahi kuhudumu kambini mwa Southampton kwa kipindi kifupi zaidi. Aliajiriwa Novemba 10, 2022 na akashuhudia kikosi hicho kikipoteza mechi tisa kati ya 14.

Rekodi hiyo duni inajumuisha kichapo katika mechi nane kati ya tisa za EPL na kichapo kingine cha mechi nne mfululizo katika uwanja wao wa nyumbani wa St Mary’s.

Jones ndiye kocha wa nane wa EPL kutimuliwa katika kipute hicho msimu huu wa 2022-23. Wakufunzi Chris Cohen na Alan Sheehan waliokuwa wasaidizi wa Jones pia wamefurushwa ugani St Mary’s huku Ruben Selles akitarajiwa sasa kusimamia pambano la EPL litakalokutanisha Southampton na Chelsea ugani Stamford Bridge mnamo Februari 18, 2023.

Jones aliaminiwa kuwa mrithi wa kocha Ralph Hasenhuttl kambini mwa Southampton mnamo Novemba 2022 baada ya kupokezwa mkataba wa miaka mitatu na nusu uliomchochea kuagana na Luton.

Alipoteza mechi nne kati ya tano za kwanza alizosimamia katika kikosi cha Southampton huku ushindi wake wa pekee katika kipindi hicho ukiwa wa 2-1 dhidi ya Lincoln katika Carabao Cup.

Ushindi mara tatu katika kipindi cha wiki moja dhidi ya Crystal Palace katika Kombe la FA, Manchester City katika Carabao Cup na Everton katika EPL, ni ufanisi uliotarajiwa kuashiria mwanzo wa ufufuo wa makali ya Southampton chini ya Jones.

Hata hivyo, kikosi hicho kilishuka zaidi na kikashuhudia msururu wa matokeo duni hadi Jones alipopigwa kalamu.

WAKUFUNZI WA EPL WALIOKOSA KUHUDUMU KWA SIKU 100

JINA LA KOCHA    KLABU  IDADI YA SIKU ZA KAZI
Les Reed Charlton Athletic 41
Rane Meulensteen Fulham 75
Frank Boer Crystal Palace 77
Bob Bradley Swansea City 84
Quique Flores Watford 85
Terry Connor Wolves 91
Nathan Jones Southampton 95
Colin Todd Derby County 98

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Napoli wapepeta wanyonge Cremonese na kufungua pengo la...

Wapenzi wa Taifa Leo waongezeka nchini – MCK

T L