• Nairobi
  • Last Updated May 20th, 2024 12:05 PM
TUK Hummer mabingwa Grandpa Super Cup

TUK Hummer mabingwa Grandpa Super Cup

Na JOHN KIMWERE

TIMU ya Chuo Kikuu cha Kiufundi cha Kenya (TUK) maarufu TUK Hummers imetawazwa mabingwa wa shindano la GrandPA Betika Super Cuo makala ya pili.

Katika fainali ya kipute hicho TUK Hummers chini ya kocha, Francis Oduor na Luke Aluoch iliibuka mabingwa wa kipute hicho baada ya kunyuka Makarios 111 (Riruta United) kwa bao 1-0 ugani Impala Club, Nairobi.

Baadhi ya wachezaji wa Makarios na viongozi wao baada ya kutuzwa kombe la nafasi ya pili kwenye shindano la GranbPA Betika Super CUP. PICHA | JOHN KIMWERE

Makarios iliyoibuka kileleni mwa mechi za makundi ilianza mchezo huo kwa mkosi baada ya beki wake kulambishwa kadi nyekundu kunako dakika ya tano.

Mchezaji wa Makarios (kulia) akishindana na mwenzake wa TUK Hummers katika fainali ya GranbPA Betika Super CUP. TUK ilishinda bao 1-0. PICHA | JOHN KIMWERE

Kwa kiwango fulani hatua hiyo ilididimiza mchezo wa kikosi hicho licha ya kuonekana kuzinduka katika kipindi cha pili.

Hata hivyo wasomi wa TUK Hummers walipata bao hilo kunako dakika ya kumi lililofunikwa kimiani na Obera Edwin.

”Tunashukuru wachezaji wetu kwa ushindi huo. Hata hivyo ni wazi kwamba wapinzani wetu walionyesha mchezo mzuri,” alisema kocha Aluoch na kuongeza kuwa kawaida lazima mshindi angepatikana.

Nayo Kibera Soccer ya Kocha Cedric Mutiva ilimaliza ya tatu baada ya kuzima wenzao wa Kibera United kwa mabao 3-1. Wafungaji wa Kibera Soccer walikuwa Anthony Oyugi mabao mawili naye Lucas Maina alicheka na wavu mara moja.

Tuzo kwa mchezaji binafsi

Kwenye tuzo za kibinafsi, Anthony Oyugi wa Kibera Soccer aliibuka mfungaji bora kwa kutikisa wavu mara 11 kitengo cha wanaume.

Mchezaji wa Gogo Boys Emmanuel Juma alituzwa mnyakaji bora katika ngarambe hiyo.

Ramadhan Vijago aliibuka kocha bora huku Enock Omari akitwaa tuzo ya mwamuzi bora.

Ramadhan Vijago akituzwa baada ya kuibuka kocha bora katika mashindano ya GranbPA Betika Super CUP. PICHA | JOHN KIMWERE
Enock Omari akituzwa baada ya kuibuka mwamuzi bora katika mashindano ya GranbPA Betika Super CUP. PICHA | JOHN KIMWERE

Nayo timu ya wachezaji wenye asilia ya Sudan Kusini ilitwaa tuzo ya kuonyesha nidhamu nzuri pia kutochelewa kufika uwanjani.

Wachezaji wa Rumanyuon FC wakipokea tuzo ya kuibuka timu yenye nidhamu ya hali ya kuu katika mashindano ya GrandPA Betika Super CUP. PICHA | JOHN KIMWERE

Nusu fainali

TUK Hummers chini ya nahodha, Evans Otieno ilicharaza Kibera Soccer kwa mabao 5-4 kupitia mikwaju ya penalti baada ya kutoka nguvu sawa bao 1-1 kwenye nusu fainali.

Katika robo fainali, TUK Hummers ilisajili ushindi wa bao 1-0 mbele ya Rumanyuon FC.

Nayo Makarios iligaragaza Kibera United mabao 5-4 kwa mipigo ya penalti baada ya kuachana kwa mabao 2-2. Makario ilikuwa imetandika Mashimoni FC kwa bao 1-0 katika fainali.

TUK Hummers ni kati ya vikosi ambavyo hushusha ushindani mkali katika michezo ya Vyuo Vikuu vya Kenya (KUSA).

TUK Hummers inajivunia kushinda taji la SportPesa Super Eight Champions League (SPS8 CL) pia SportPesa Super Eight League (SPS 8).

Aidha iliwahi kumaliza ya pili kwenye mechi za S8PL na S8PL CL.

Kando na soka chuo cha TUK kina timu za fani mbali mbali ikiwamo Raga, Karate, Tae kwo Ndo, JUDO, Vikapu, Voliboli, mpira wa mikono, Mashindano ya Mbio na Hoki kati ya nyingine.

 

You can share this post!

Aubameyang apokonywa utepe wa unahodha kambini mwa Arsenal

Mufya yatwaa taji la Patrick Oboya Cup

T L