• Nairobi
  • Last Updated May 21st, 2024 7:05 PM
Tundo ndiye mfalme wa KCB Thika Rally

Tundo ndiye mfalme wa KCB Thika Rally

Na GEOFFREY ANENE

DEREVA Carl “Flash” Tundo alihifadhi ubingwa wa duru ya Mbio za Magari za Kitaifa za Kenya (KNRC) ya KCB Thika Rally katika kaunti ya Kiambu hapo jana.

Tundo, ambaye alitwaa ubingwa wa KCB Micro Banking Rally katika kaunti ndogo ya Thika mara ya mwisho duru hiyo iliandaliwa mwaka 2009, alitwaa ushindi wake wa nne msimu huu alipokamilisha kilomita 142.18 za makala ya 2021 kwa saa 1:47:09.1.

Akishirikiana na mwelekezi wake Tim Jessop katika gari la Mitsubishi Lancer Evolution 10, alibwaga mpinzani wake mkuu Baldev Chager kwa 29.4.Drama ilishuhudiwa katika mkondo wa kwanza (Bufallo 1) wa kilomita 30.52 pale baadhi ya madereva wawili wa kwanza Issa Amwari na Jasmeet Chana walipotea njia.

Tundo alimaliza mkondo huo katika nafasi ya tano kabla ya kurukia uongozi alipotawala mkondo wa pili (Ananas 1) wa kilomita 21.69 kwa dakika 34:07.6, sekunde 2.3 mbele ya mpinzani wake mkuu Baldev Chager pamoja na Jasmeet Chana na makinda Hamza Anwar na McRae Kimathi mtawalia.

Tundo, ambaye mwaka huu umempenda akishinda taji la Afrika pamoja na duru za kitaifa za Equator Rally, Machakos Rally na Nanyuki Rally, alisalia kileleni katika mkondo wa tatu (Pavillion 1) wa kilomita 3.09 nao Chana, Aakif Virani, Kimathi, Hamza na Chager wakimfuata unyounyo katika usanjari huo.

Chager alitetemesha katika mkondo wa nne (Ndula 1) wa kilomita 25.68 akifuatiwa na Tundo, Chana, Kimathi na Maxime Wahome mtawalia.Pia, Chager alitawala mkondo wa tano (Bufallo 2) wa kilomita 31.13 akifuatiwa na Tundo, Kimathi, Chana na Wahome mtawalia.

Chager alitesa katika mkondo wa sita (Pavillon 2) wa kilomita 3.09 akifuatiwa na Tundo, Chana, Kimathi na Wahome mtawalia. Ingawa Chager pia alishinda mkondo wa mwisho (Ndula 2 Power Stage), Tundo, ambaye alimaliza mkondo huo nambari mbili, alikuwa amefanya ya kutosha kutwaa taji ya KCB Thika Rally iliyoanzia katika Chuo Kikuu cha Mount Kenya na pia kumaliza mle.

Duru ya mwisho ni Guru Nanak Rally mwezi ujao. Matokeo ya KCB Thika Rally mnamo Novemba 21 (saba-bora): Carl Tundo/Tim Jessop (Mitsubishi Evo 10) saa 1:47:09.1, Baldev Chager/Ravi Soni (Volkswagen Polo) 1:47:38.5, Jasmeet Chana/Ravinder Chana (Mitsubishi Evo 10) 1:52:15.5, McRae Kimathi/Mwangi Kioni (Ford Fiesta) 1:56:58.5, Maxime Wahome/Linet Ayuko (Subaru Impreza) 2:03:32.1, John Ng’ang’a/Edward Ndukui (Subaru Impreza) 2:13:14.6, Daren Miranda/Amman Shah (Subaru Impreza) 2:19:13.5.

You can share this post!

Hatimaye mwafaka wapatikana Sudan

Kheri ashauri vituo vya soka ya vijana vifufuliwe

T L