• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 11:33 PM
Wakenya waanza kuvuna medali michezo ya walemavu ya Dubai Grand Prix

Wakenya waanza kuvuna medali michezo ya walemavu ya Dubai Grand Prix

NA GEOFFREY ANENE

KENYA hatimaye imeshinda medali kwenye riadha za kimataifa za walemavu za Dubai Grand Prix baada ya kuvuna dhahabu, fedha mbili na shaba katika siku ya tatu nchini Milki za Kiarabu, Jumatano.

Nancy Chelangat ameshindia Kenya nishani ya dhahabu katika mbio za mita 400 T/11 baada ya kukamilisha umbali huo kwa dakika 1:04.25. Raia wa India, Ishwari Nishad ameridhika na medali ya fedha kwa 1:25.50. Kitengo hicho kilichovutia washiriki watatu kilishuhudia raia wa Colombia, Ionis Salcedo akikosa medali kwa sababu ya kuvunja sheria za mashindano.

James Onyinka Mangerere ametwaa medali ya fedha katika urushaji wa mkuki katika kitengo cha F/57 wanaotumia viti vya magurudumu. Mwanariadha huyo mwenye umri wa miaka 36 ameandikisha mtupo wa mita 38.65, sawa na Sakchai Yimbanchang kutoka Thailand. Mohamad Mohamad kutoka Syria amenyakua dhahabu akiwa amerusha mkuki umbali wa mita 41.93. Kitengo hicho kilivutia washiriki saba.

Nelly Nasimiyu Munialo, 37, ameridhika na nishani ya shaba mbio za mita 400 T12/13 baada ya kutimka umbali huo kwa dakika 1:08.50 akimaliza nyuma ya Wafaransa Celia Terki kutoka Uturuki (1:03.56) na Lucile Razel (1:04.50).

Henry Nzungi ametia kapuni nishani ya fedha mbio za mita 400T12 kwa dakika 1:02.50, huku raia wa Colombia Yamil Davi akitwaa dhahabu kwa sekunde 50.48.

John Njoroge Mukiri,35, pia alipoteza alama kwa kuenda kinyume na sheria za mashindano katika mbio za mita T11. Kenya iliingiza wanariadha 19 katika mashindano hayo yaliyoanza Machi 21. Yatakamilika Machi 24.

  • Tags

You can share this post!

Kampeni: IEBC yapendekeza Ruto na Raila wachunguzwe

N’Golo Kante ajiondoa katika timu ya taifa ya...

T L