NA PATRICK KILAVUKA
YOUNG City Academy sasa yasajili makinda wake wa soka kujijengea shina la timu.
Tayari imesajili wachezaji arubani walio na chini ya miaka 13 na 15.
Academy hii ambayo ilianza karibu mwaka mmoja unusu umepita, inazaidi kuwavutia chipukizi wengine kila uchao kutokana na mikakati bora ya kuboresha talanta chini ya mwanzilishi wake kocha Dickson Amugashia.
Anamshirikisha mkufunzi msaidizi Jackson Namu kuunga timu ya chipukizi ambayo itakuwa na talanta za kuvutia timu za hadhi nchini na nje kwa minajili ya kujitanua zaidi.
Madhumuni ya kuianzisha yalikuwa; kuwawezesha wanatalanta kuwavutia wafadhili wa masomo kwani kuna shule zinahitaji wanavipaji wa soka kuwadhamini masomo. Mbali na kujenga jina la shule husika. Pia, akademia inanuia kukomboa vijana wajiepushe na utovu wa nidhamu. Isitoshe, kukuza na kulea talanta pamoja na kuimarisha mahusiano bora katika jamii.
Imeungwa mkono na wazazi kwa sababu wameweza kushirikiana na wadau kuhakikisha kwamba, wachezaji hawa wanalelewa vipaji katika mazingira mema na wanawafuatilia uwanjani. Jambo hilo, huwa la kuwatia motisha wachezaji zaidi.
Nahodha Ignatius Chakuri wa akademia hii, anasema anashirikiana na wachezaji wenza kuona kwamba wanajenga umoja ulio nguvu ya timu mbali na kutia bidii ya mchwa katika kufanya mazoezi na nidhamu kuwa ada. Hata hivyo, yeye amepata ufadhili wa masomo kupitia talanta.
Mazoezi ambayo ni kiungo bora kwa mchezaji kuwa hodari, yanafanywa kila wikendi wakati shule zimefunguliwa, japo wakati wa holidei au likizo hufanywa kila siku.
Wakati wa kujinoa, wanasoka chipukizi hawa wanahamasishwa na kufunzwa kuhusu jinsi ya kugundua nafasi zao uwanjani, kupokea mpira, kuzunguka, kuvizia, kudhibiti, kupiga pasi, kuchenga, kupepeta miongoni mwa stadi nyingine kusakata boli
Wachezaji ambao wameanza kutoa makucha ya kabumbu wakati timu hii inajengwa kulingana na kocha aliye pia msimamizi Amugashia ni kiungo Allvin Asunga, Difenda David Kisanya, straika Bramwell Thoya miongoni mwa wengine ambao mwamo mkondoni.
Wamejiangazia katika kipute cha TICK-TACK ambapo walifika robo fainali na kuondolewa na Wasafi kwa matuta 7-6 baada ya kuagana sare tasa katika muda wa kawaida.
Mipango ya akademia sasa ni kuzidi kutoa vifaa bora vya kimaadili na vilivyo tayari kucheza soka nje na ndani ya nchini. Hususan wanalenga ligi ya FKF na vipute kama jukwaa la kuviangazia vipawa hivi.