TITUS OMINDE Na CECIL ODONGO
RAIS William Ruto amewataka viongozi wa upinzani wakome kumhangaisha kuhusiana na ahadi alizotoa wakati wa kampeni zilizoishia katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9.
Kiongozi wa nchi alisema kuwa anafahamu kila ahadi aliyoitoa akisisitiza kuwa atahakikisha amezitimiza zote.
Alitaka upinzani umpe muda wa kutekeleza ahadi hizo badala ya kumpa shinikizo kila mara ilhali serikali yake “inachapa kazi”.
Wiki jana, kinara wa upinzani, Bw Raila Odinga alitoa taarifa ya kutathmini utendakazi wa Serikali katika siku 100 ambazo imekuwa mamlakani.
Bw Odinga alisema utawala wa Kenya Kwanza umewasababishia Wakenya maumivu na kilio kwa kuwa “imeanza kubadili nia katika utekelezaji wa ahadi ilizotoa wakati wa kusaka kura”.
Bw Odinga alikosoa utawala wa sasa kwa “kuzidisha ugumu wa maisha” na kuipa asilimia 40 pekee katika utendakazi.
Bw Odinga tayari ametangaza kuwa atawapa wafuasi wake mwelekeo wa kisiasa Januari 2023 kama sehemu ya mikakati ya kuisukuma serikali iwajibikie raia.
Akizungumza katika ibada ya pamoja iliyoandaliwa na makanisa mbalimbali siku ya Krismasi katika uwanja wa Eldoret Sports Club, Kaunti ya Uasini Gishu, Rais Ruto alisema kuwa serikali ya Kenya Kwanza ilirithi uchumi ambao ulisambaratika na anahitaji muda wa kuufufua.
Alidai kuwa Kenya iko pabaya kwa sababu uchumi wake ulisambaratishwa na ukuruba kati ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta na Bw Odinga kati ya 2018-2022.
Japo alikiri kuwa upinzani unatekeleza wajibu muhimu wa kuukosoa utawala wake, Rais alisema itachukua muda zaidi kuondoa ‘uchafu’ aliourithi kutoka kwa serikali iliyopita.“Nimeamua kuwa kabla ya kuyashughulikia mambo mengine, jambo la kwanza ambalo lazima nimakinikie ni kujenga uchumi wetu upya. Nyinyi mnafahmu kuwa uchumi wetu kwa sasa uko pabaya. Serikali iliyopita ilikuwa inatumia asilimia 65 ya mapato yetu kulipa mkopo wa Sh1.4 trilioni kila mwaka,” akasema Rais Ruto.
“Nawaambia wale ambao wanajaribu kunihangaisha waje polepole. Sote tupange na kuweka mikakati ya kubuni msingi wa uchumi imara ili tunufaike badala ya kuwa na nchi ambayo inaendeshwa kwa madeni,” akaongeza.
Ingawa alitambua kuwa ushirikiano katika kuendeleza taifa na upinzani ni jambo linalostahili, Rais kwa mara nyingine alisema hatakubali kuingia kwenye “salamu ya maridhiano” na Bw Odinga almaarufu handisheki jinsi alivyofanya Rais Kenyatta katika kipindi cha pili cha utawala wa Jubilee.
“Furaha yangu ni kuwa tuna upinzani ambao unatekeleza vyema jukumu lake la kuitia kwenye mizani serikali. Wao wafanye kazi yao nasi pia tutekeleze yetu kwa kuwa ni wajibu wa kila upande kikatiba,” akasema Rais.
Alipomkosoa Rais wiki jana, Bw Odinga alisema licha ya ziara nyingi ambazo Kiongozi wa Nchi amefanya katika nchi za kigeni, hakuna lolote la maana aliloafikia ili kuiondolea nchi mzigo mkubwa wa madeni.
Waziri huyo mkuu wa zamani alishangaa kwa nini Rais hajazungumza na China na Amerika ambazo zinaidai Kenya madeni makubwa jinsi alivyoahidi wakati wa kampeni.
Ibada hiyo ya siku ya Krismasi ilikuwa hafla ya kwanza kwa Rais Ruto katika kaunti hiyo yake ya nyumbani tangu achukue uongozi wa nchi.
Ikizingatiwa kuwa Uasin Gishu na kaunti jirani ya Trans Nzoia huchukuliwa kuwa “ghala” la taifa kutokana na kunawiri kwa kilimo cha mahindi, Rais aliwaahidi wakulima kuwa bei ya mbolea itaendelea kushuka kutoka kwa bei ya sasa ya Sh3,500.
Alishikilia kuwa kupunguza bei ya mbolea na pembejeo nyingine za kilimo, kutasaidia Kenya kujitosheleza kwa chakula badala ya serikali kutumia pesa nyingi katika kupunguza bei ya unga jinsi serikali iliyopita ilikuwa ikifanya.
Hata hivyo, aliwataka wakulima ambao bado wanayahodhi mahindi wayauze kwa Bodi ya Kitaifa ya Nafaka (NCPB) kabla ya Februari 2023 ambapo serikali itaanza kuagiza mahindi nje ya nchi.
Subscribe our newsletter to stay updated