• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 7:05 PM
Azimio kuwapa wafuasi mwelekeo Septemba

Azimio kuwapa wafuasi mwelekeo Septemba

KASSIM ADINASI Na SIMON CIURI

KIONGOZI wa Azimio La Umoja-One Kenya Raila Odinga amewataka wafuasi wa muungano huo wasubiri mwezi huu wa Agosti utamatike kabla ya kufahamishwa mkondo mwingine wa kufuata.

Bw Odinga ambaye amekuwa akihutubu katika eneobunge la Gem, Kaunti ya Siaya katika hafla ya mazishi ya David Omondi Ofwaya, amesema mrengo tawala wa Kenya Kwanza unapewa muda huo wa mwezi mmoja kufanya mazungumzo ya maridhiano na Azimio.

“Kenya Kwanza wana muda wa mwezi mmoja kuzungumza nasi. Ikiwa hatutakubaliana, tutawapa watu wetu mwelekeo mnamo Septemba 1, 2023,” amesema Bw Odinga.

Na wakati huo huo, dalili za vuta nikuvute sasa zinaanza kujitokeza baada ya Rais William Ruto kwenye ziara yake katika eneo la Mlima Kenya kusisitiza Jumamosi kwamba atawakalia ngumu wapinzani.

Rais Ruto ambaye amewahutubia wakazi wa Githurai 45, eneobunge la Ruiru, Kaunti ya Kiambu, amesisitiza hakutakuwa na handisheki.

“Wanapoteza muda kwa kuleta vitisho vya kutaka handisheki. Hao watu nitawakalia ngumu sana,” amesema Rais Ruto.

Kiongozi wa nchi amewaahidi wakazi kwamba masoko mengine 15 yatajengwa katika Kaunti ya Kiambu.

Vile vile ameahidi kwamba pesa zaidi zitaelekezwa katika sekta ya elimu.

Kuhusu kupanda kwa gharama ya maisha, Rais amesema manifesto ya Kenya Kwanza inaweka wazi mikakati ya kurahisisha maisha ya Wakenya ambao kwa kweli wamelemewa na mzigo wa maisha.

Amechukua fursa hiyo kufafanua kwamba ujenzi wa nyumba za gharama nafuu utasaidia pakubwa kukabili tatizo la ukosefu wa ajira.

“Si tulisema Kazi Ni Kazi ama nyinyi ni wale wa kuchagua kazi?” akauliza.

Rais vile vile amewahutubia wakazi wa Kenol (Murang’a) na Kagio (Kirinyaga).

  • Tags

You can share this post!

JAGINA WA SPOTI: Alitikisa soka Harambee Starlets sasa ni...

Waiguru na Wangui Ngirici wazika tofauti zao

T L