Na Wycliffe Nyaberi
NAIBU Rais William Ruto huenda akakosa uungwaji mkono katika eneo la Gusii iwapo Waziri wa Usalama Dkt Fred Matiang’i atawania Urais 2022.
Naibu Gavana wa Kisii Joash Maangi ambaye ni mwandani wa Dkt Ruto, jana alisema kuwa atamuunga mkono Dkt Matiang’i akiwania.
Bw Maangi, ambaye amekuwa akiendesha shughuli zote za chama cha United Democratic Alliance (UDA) katika eneo la Gusii, alisema hayo siku mbili baada yake na wanasiasa wengine wa Tangatanga kutoka kaunti za Nyamira na Kisii, kukutana na Dkt Ruto jijini Nairobi, Alhamisi.
“Unajua mimi nalenga kuwa gavana wa Kisii na iwapo ‘mtoto’ wetu Matiang’i atawania urais, bila shaka jamii yote itakuwa nyuma yake na haitamsikiza mtu yeyote atakayekwenda kinyume. Nitaonekana mtu mjinga kumpinga kwani huo utakuwa mwisho wangu kisiasa na nitatumwa kijijini mapema asubuhi,” akasema Bw Maangi.