• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 11:29 AM
Natembeya ajitosa rasmi kusaka ugavana Trans Nzoia

Natembeya ajitosa rasmi kusaka ugavana Trans Nzoia

Na GERALD BWISA

MSHIRIKISHI Mkuu wa eneo la Bonde la Ufa, Bw George Natembeya, amejiunga rasmi kwenye kinyang’anyiro cha ugavana katika Kaunti ya Trans Nzoia, huku akiahidi kuiboresha kaunti hiyo katika nyanja zote.

Mkuu huyo, ambaye anatarajiwa kujiuzulu wadhifa wake wiki hii, atakabiliana na zaidi ya watu kumi, ambao wametangaza nia ya kuwania nafasi hiyo.

Kwa miezi sita iliyopita, Bw Natembeya amekuwa akizuru sehemu mbalimbali katika kaunti hiyo kuvumisha azma yake kwa wenyeji.

Anawindwa na vyama vya ODM na Democratic Action Party (DAP-K), kinachohusishwa na Waziri wa Ulinzi, Eugene Wamalwa.

Wiki iliyopita, Katibu Mkuu wa ODM, Bw Edwin Sifuna, alimwalika Bw Natembeya kujiunga na chama hicho, ili kupigania tiketi yake na wawaniaji wengine ambao wametangaza azma zao.

Bw Sifuna alikuwa kwenye ziara ya kukipigia debe chama katika kaunti hiyo.

“Nitajiuzulu rasmi na kuanza kampeni zangu kuwarai wakazi kunipigia kura kama gavana wao wa pili,” akasema Bw Natembeya, kwenye mahojiano na Taifa Leo.

Mbunge wa Kiminini, Chris Wamalwa pia ametangaza nia ya kuwania nafasi hiyo.

Amekuwa akimshinikiza Bw Natembeya kujiuzulu wadhifa wake na kujiunga rasmi kwenye kivumbi hicho.

Bw Natembeya ameahidi kuboresha sekta ya afya kwa kupanua vituo vya afya vilivyopo katika kila wadi kuwawezesha wenyeji kupata huduma bora.

You can share this post!

TUSIJE TUKASAHAU: Ripoti yasema kaunti zote 47 zinadaiwa...

Wanasiasa watia Haji presha kali

T L