• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Sababu ya Mariga kuruhusiwa kujaribu bahati Kibra

Sababu ya Mariga kuruhusiwa kujaribu bahati Kibra

NA SAMUEL OWINO

KORTI inayoshughulikia mizozo ya uchaguzi Jumatatu ilimruhusu aliyekuwa kiungo matata wa timu ya taifa ya kandanda McDonald Mariga kuwa debeni katika uchaguzi mdogo wa eneobunge la Kibra.

Awali, uteuzi wake na chama cha Jubilee ulikuwa umetupiliwa mbali na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwa kuwa taarifa muhimu kumhusu zilikosekana katika orodha ya wapigakura walioshiriki uchaguzi mkuu wa 2017.

Hata hivyo, mwenyekiti wa IEBC Bw Wafula Chebukati, ametangaza Jumatatu kuwa Mariga sasa anaweza kuwania kiti hicho kilichosalia wazi baada ya kifo cha Bw Ken Okoth hapo Julai.

Bw Chebukati amesema mkuu wa uchaguzi eneebunge hilo aliyemzuia Mariga kuwa debeni alisahau kuangalia orodha mpya ya mwaka huu katika eneobunge la Starehe.

Kundi la mawakili waliomwakilisha Bw Mariga, likiongozwa na Elisha Ongoya, liliirai IEBC kusahihisha kosa hilo nakumruhusu mwanaspoti huyo kujaribu bahati yake uchaguzini.

“Simlaumu afisa wa uchaguzi kwa kufanya kosa hilo. Lakini lazime lingesahihishwa na kamati ya uchaguzi ili kuwapa wapigakura wa Kibra nafasi murua ya kuchagua wamtakaye,” akasema.

Aliongeza kuwa Mariga ametimiza masharti yote ya kikatiba kuhusu uchaguzi, akieleza kuwa mwaniaji anapaswa kuwa amesajiliwa kuwa mpiga kura, na mchckato huo huendelea hata wakati hakuna uchaguzi.

Kwa sasa, Bw Mariga ana nafasi ya kujiunga na wanasoka wengine duniani ambao waling’aa kwa siasa baada ya kustaafu kucheza gozi.

Miongoni mwao ni aliyekuwa straika wa Inter Milan na Chelsea Andriy Shevchenko, mshindi wa Kombe la Dunia la 1994 Romario na aliyekuwa straika matata wa PSG,  AC Milan na Monaco George Weah, ambaye sasa ni rais wa Liberia.

Mariga amesema sasa yuko tayari kuogelea katika bahari ya siasa akiusifu uamuzi wa Bw Chebukati.

“Namshukuru Maulana kwa mchakato wa leo. IEBC imenitendea haki. Kwa sasa najitosa kwa kampeni ili niwashawishi wapigakura wa Kibra,” akasema.

 

You can share this post!

Poghisio amkejeli Lonyangapuo kubadilisha mawaziri kila mara

Thamini wateja wako, mkuu wa Username ashauri baada ya tuzo

adminleo