NA WAANDISHI WETU
USHINDI wa Bw Abdulswamad Nassir kuwa gavana wa pili wa Mombasa, umezima nia ya Chama cha UDA kinachoongozwa na rais mteule, Dkt William Ruto, kudhibiti uongozi wa kisiasa katika kaunti hiyo.
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), jana Jumanne ilimtangaza Bw Nassir mshindi wa uchaguzi huo uliokuwa umeahirishwa mara mbili.
Mwanachama huyo wa ODM alizoa kura 119,083 dhidi ya mpinzani wake wa karibu, Bw Hassan Omar, aliyepata kura 98,105 kupitia UDA.
Kinyang’anyiro cha kushindania urithi wa gavana anayeondoka, Bw Hassan Joho, kilivutia ushindani mkali kati ya ODM inayoongozwa na Bw Raila Odinga, na UDA.
Kwa upande mmoja, ODM ilikuwa na mtihani kudhihirisha bado kaunti hiyo ni ngome ya Bw Odinga kisiasa, huku Dkt Ruto akijitahidi kung’oa mizizi ya chama hicho cha chungwa Pwani.
Juhudi za UDA ziliambulia patupu kwani chama hicho cha wilbaro kilifanikiwa kuzoa kiti kimoja pekee cha ubunge huku ODM ikipata viti vitano vya ubunge, kile cha useneta, mwakilishi wa kike bungeni mbali na ugavana na wingi wa viti vya udiwani.
Akizungumza baada ya kupokea cheti chake cha ushindi, Bw Nassir alitoa wito kwa wapinzani wake kuungana naye ili kuendeleza mbele kaunti hiyo.
“Hizi siasa kuanzia leo zimemalizika. Niko tayari kufanya kazi na yeyote ambaye nia yake haikuwa matusi bali kuendeleza mbele Mombasa,” akasema.
Alikuwa ameandamana na wanasiasa wengi wa Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya akiwemo Bw Joho, Mwenyekiti wa chama, Bw John Mbadi, aliyekuwa gavana wa Kitui, Bi Charity Ngilu, Mbunge wa Embakasi Mashariki, Bw Babu Owino, miongoni mwa wengine.
Baadhi ya viongozi wa Kenya Kwanza katika Kaunti ya Mombasa akiwemo Mbunge wa Nyali, Bw Mohamed Ali, aliyekuwa gavana wa Nairobi, Bw Mike Sonko, na aliyekuwa mbunge wa Kisauni, Bw Ali Mbogo, walikubali matokeo.
Bw Sonko ambaye alihamia Kenya Kwanza kutoka Azimio baada ya kuzuiwa kuwania kiti hicho, alisema sasa ataendelea kuhudumia wananchi kupitia kwa kikundi chake cha Sonko Rescue Team.
Bw Nassir sasa ana kibarua kutekeleza kikamilifu ahadi ambazo alitolea wakazi wa jiji hilo wakati wa kampeni zake.
Baadhi ya changamoto sugu zilizo Mombasa ni kuhusu uzoaji wa takataka, usambazaji maji safi ya mifereji mitaani, kucheleweshwa kwa mishahara ya wafanyakazi wa kaunti ambayo ni hali inayosababisha migomo mara kwa mara, na malalamishi kuhusu ada za juu za kufanya biashara ambayo husemekana kuathiri nafasi za ajira na ujasiriamali.
“Nimemwambia Joho ile miradi aliyoanza ni jukumu langu kukamilisha. Mahali kulikuwa na makosa turekebishe, palipokuwa na mazuri tuendeleze,” akasema Bw Nassir.
Katika Kaunti ya Kakamega, Bw Fernandes Barasa wa ODM alitangazwa mshindi wa ugavana kwa kupata kura 192,929 dhidi ya Bw Cleophas Malala wa ANC aliyepata kura 159,508.
Bw Malala alikubali matokeo hayo akisema inafaa viongozi wajitolee kukubali matokeo hata kama hayaegemei upande wao.
Subscribe our newsletter to stay updated