NA MARY WANGARI
VIONGOZI wa Azimio la Umoja One Kenya wamekanusha vikali madai ya migawanyiko baina ya uongozi na vyama tanzu vya muungano huo wa upinzani.
Wakihutubia wanahabari jana Jumatatu katika majengo ya Bunge, walipuuzilia mbali ripoti za kuwepo njama ya kumtimua Seneta wa Isiolo, Fatuma Dullo, kama Naibu Kiranja wa Wachache.
Wakiongozwa na Kiongozi wa Wachache, Seneta wa Kilifi Stewart Madzayo, viongozi wa Azimio waliwahakikishia wafuasi wao kuwa Muungano huo ungali imara na kwamba tofauti zote zilizokuwepo zimesuluhishwa.
“Tumeshiriki majadiliano ya kina na vinara wetu: Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta, Raila Odinga na Kalonzo Musyoka na tunataka kuweka wazi kuwa kama Azimio tungali pamoja. Hakuna mgawanyiko kila kitu kimeshughulikiwa na hapana haja ya kuwa na hofu,” alisema Seneta Madzayo.
Seneta huyo aliandamana na Maseneta Ledama Ole Kina (Narok) Enoch Wambua (Kitui) na Seneta Dullo ambaye jina lake lilitupiliwa mbali kwenye orodha ya waliopendekezwa kwa nyadhifa za Tume ya Huduma za Bunge (PSC).
Kufuatia Mswada uliopitishwa bila kupingwa na Seneti na Bunge la Kitaifa, jina la Seneta Dullo liliondolewa na nafasi yake kujazwa na Seneta wa Nyamira Erick Okongo Omogeni, hatua iliyoibua hisia kali kutoka kwa Jubilee iliyotishia kujiondoa katika Azimio.
Awali, Seneta Madzayo alisema alimwandikia Spika wa Seneti Amason Kingi akimtaka kupuuzilia mbali barua iliyokuwa imeandikwa baadhi ya wanachama wa Azimio waliompendekeza Bi Dullo, hatua iliyoashiria migawanyiko katika Muungano huo.
Hata hivyo, akizungumza jana Jumatatu kuhusu barua hizo mbili zilizoonekana kukinzana, Seneta Dullo alisisitiza kuwa viongozi wa Azimio wangali wanazungumza kwa sauti moja.
“Hakukuwa na tofauti zozote hata katika barua hizo mbili tofauti zilizotumwa jana. Katika kiwango cha uongozi hakuna mivutano na ikiwa kuna masuala tata yoyote, yatasuluhishwa kinyumbani,” alisema Bi Dullo.
Viongozi hao walichelea kuzungumzia kuhusu uteuzi katika Bunge la Afrika Mashariki (EALA) wakiutaja kama “siasa za mapema.”
Haya yanajiri huku Azimio ikionekana kuyumbishwa na uwaniaji wa nyadhifa muhimu baina ya vyama wanachama ambapo ODM imeshutumiwa kwa kujitwalia vinono katika kamati muhimu za Bunge, PSC na (EALA).
Azimio imegubikwa na hali ya kutojali na usaliti huku wanasiasa mashuhuri kutoka mrengo huo wakionekana kuendeana kinyume.
Wiki iliyopita, Katibu Mkuu wa ODM, Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, alifichua kuhusu njama za kumng’atua Seneta Dullo kutoka kwa wadhifa wake wa naibu Kiranja wa Wachache.
Seneta Sifuna alidai kuwa maseneta 22 miongoni mwa 29 wa Azimio tayari wametia saini pendekezo la kumbandua Bi Dullo huku akimtaka ajiuzulu kwa hiari la sivyo ang’atuliwe.
Kupitia akaunti yake kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, Bw Sifuna alichapisha ujumbe ulioashiria mgawanyiko mkali katika Azimio.
“Mdahalo na ndugu zetu kutoka Jubilee kuhusu utapeli ni jambo ambalo ninasubiri kwa hamu,” alisema.
Subscribe our newsletter to stay updated