SHANGAZI;
Nimekuwa na uhusiano wa kimapenzi na pasta wa kanisa langu. Nina mimba yake lakini amenikana. Hujifanya matakatifu sana na hata nikiambia watu hakuna anayeweza kuniamini. Nifanyeje?
Pasta pia ni binadamu na anaweza kunaswa na kutumiwa na shetani. Sielewi uhusiano wenu ulianzaje hadi ukafikia hapo. Unafaa kujilaumu kwa matokeo hayo pia. Sasa amekuhepa na itabidi ubebe mzigo huo.
Mwanamke ambaye nimekuwa nikimtaka kwa miaka miwili alinitumia ujumbe juzi akaniambia yuko tayari kuwa mpenzi wangu. Nimepata mwingine ambaye nampenda hata zaidi. Nifanyeje?
Sidhani unahitaji ushauri wangu ili kuamua kuhusu jambo hilo. Kama umepata ambaye umetosheka kuwa ndiye chaguo la moyo wako, itabidi umwambie huyo mwingine ingawa uamuzi huo utamvunja moyo.
Nina umri wa miaka 31 na sijawahi kuwa na mpenzi maishani kwa kuwa sina hisia zozote kwa wanawake. Marafiki zangu, wakiwemo wanawake, wamekuwa wakinicheka kuhusu hali yangu hiyo. Nifanyeje?
Una sababu ya kuwa na wasiwasi kwani hiyo si hali ya kawaida. Katika umri wako huo unafaa kuwa na mpenzi na pia marafiki wengine wanawake. Tafuta mtaalamu wa afya ya uzazi uone kama atakusaidia.
Nina umri wa miaka 30. Nimeamua sitaki mpenzi na sitaolewa kwa sababu siwezi kumwamini mwanamume yeyote. Lakini nahitaji wa kunipa raha tu na sitaki kupata mimba. Waonaje?
Wewe sasa ni mtu mzima na una haki ya kuishi maisha unayotaka. Umeamua kuishi hivyo kwa sababu zako. Kama unahitaji mwanamume na hutaki mimba, basi itabidi mtumie kinga.