• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 5:50 AM
Wenyeji watumai kuzima mzozo na wasimamizi wa ‘shamba la Ruto’

Wenyeji watumai kuzima mzozo na wasimamizi wa ‘shamba la Ruto’

Na LUCY MKANYIKA

MZOZO kati ya jamii za Kaunti ya Taita Taveta na wasimamizi wa shamba linalohusishwa na Naibu Rais William Ruto, umepata matumaini kutatuliwa.

Hii ni baada ya wasimamizi wa shamba hilo kukubali shughuli za kuzibua mikondo ya mito inayoingiza maji katika Ziwa Jipe ziendelee.

Wasimamizi hao wa shamba la Kisima wakiongozwa na Bw Aries Dempers, wamekubali shughuli hiyo ianze ndani ya shamba hilo la ekari 1,000.

Wakazi kwa muda mrefu walikuwa wamelalamika kuwa shamba hilo linasababisha uwezekano wa ziwa kukauka kwa vile mikondo inayoelekeza maji ziwani ilikuwa imezibwa.

Mnamo Jumapili, kamati iliyojumuisha Diwani wa Wadi ya Mata, Bw Chanzu Kamadi, wakulima, wavuvi na wasimamizi wa shamba hilo walikutana na kuelewana kuhusu jinsi shughuli hiyo itatekelezwa.

“Tumeelewana kazi ianze Jumatatu (jana) asubuhi. Wasimamizi wameturuhusu kwa hivyo kwa sasa hakuna changamoto zimeibuka,” akasema Bw Kamadi.

Serikali ya kaunti kupitia kwa Hazina ya Ustawishaji Wadi ilitenga Sh5 milioni kuzibua mikondo ya mito ya Sombasomba, Sembike, Lesesia na Maloja ili kuongeza kiwango cha maji ziwani.

Shughuli hiyo ilichelewa kwa sababu ya mzozo kati ya wasimamizi wa shamba na wenyeji, iliposemekana wasimamizi hao walifunga sehemu zilizotakikana kufanyiwa ukarabati.

Bw Kamadi alisema shughuli hiyo inatarajiwa kukamilishwa baada ya siku 14.

Dkt Ruto amekuwa akitembelea shamba hilo mara kwa mara na hata kufanya mikutano hapo na viongozi wa kijamii.

Zamani lilikuwa likimilikiwa na aliyekuwa mbunge wa Taveta, Bw Basil Criticos.

You can share this post!

Spurs wamvizia kocha Paulo Fonseca kuwa mrithi wa Jose...

Brazil waanza vyema kampeni za Copa America kwa kucharaza...