Na GEOFFREY ANENE
TIMU ya raga ya wachezaji saba kila upande ya Kenya maarufu kama Shujaa imekutanishwa na Amerika inayotiwa makali na kocha Mike Friday kwenye duru ya Dubai Sevens ya Raga za Dunia 2021-2022 itakayofanyika nchini Milki za Kiarabu mnamo Novemba 26-27.
Katika Kundi B, mabingwa hao wapya wa Safari Sevens pia watamenyana na wakali wa Argentina na Uhispania iliyosikitisha kwenye Safari Sevens jijini Nairobi mwezi uliopita.
Vijana wa kocha Innocent “Namcos” Simiyu wataanza kampeni ya Dubai Sevens dhidi ya Amerika ambayo ilipepeta Kenya 19-14 katika mechi za makundi kwenye Olimpiki jijini Tokyo nchini Japan mwezi Julai.
Mchuano huo utasakatwa saa tatu asubuhi na dakika 16 mnamo Novemba 26. Shujaa itavaana na Argentina saa saba na nusu mchana halafu ikamilishe siku ya kwanza dhidi ya Uhispania saa kumi na dakika mbili jioni.
Kenya ilimaliza msimu 2021 katika nafasi ya tatu nchini Canada nyuma ya mabingwa Afrika Kusini na nambari mbili Uingereza baada ya kufika fainali ya Vancouver Sevens na kumaliza nambari tatu duru ya Edmonton Sevens.
Simiyu anapanga kutangaza kikosi cha kuenda Dubai mnamo Ijumaa.
Makundi ya Dubai Sevens:
Kundi A: Fiji, Australia, Canada, Ufaransa
Kundi B: Argentina, Amerika, Kenya, Uhispania
Kundi C: Afrika Kusini, Ireland, Great Britain, Japan
Ratiba ya mechi za Shujaa (saa ya Afrika Mashariki):
Novemba 26
Shujaa na Amerika (9.16am)
Shujaa na Argentina (1.30pm)
Shujaa na Uhispania (4.02pm)