• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 10:44 AM
Barobaro aliyemfuata shugamami kwake nyumbani atumiwa majibwa

Barobaro aliyemfuata shugamami kwake nyumbani atumiwa majibwa

VIPINGO, MALINDI

NA JANET KAVUNGA

BAROBARO aliyemfuata shugamami kwake baada ya kutofautiana nusra atafunwe na majibwa saba walioachiliwa na mumama huyo.

Jamaa hakuridhika mama huyo alipokatiza uhusiano wao kwani alikuwa akifaidika sana kifedha. Akamfuata hadi kwake naye akafungulia mbwa hao wakali.

Ilikuwa ni mguu niponye lakini kwa bahati nzuri, bawabu wa boma la mama huyo wa Kizungu aliwazuia mbwa hao kabla hawajamrukia polo na kumrarua.

***

Pasta mazishini asuta waombolezaji wanafiki

NAROK KUSINI

NA NICHOLAS CHERUIYOT

VITI viligeuka kuwa moto pasta alipokemea waombolezaji kwa kufurika mazishini ilhali hawakumsaidia mwendazake alipokuwa hai kukabiliana na ugumu wa maisha.

“Alipanga harambee lakini ni wachache walijitokeza. Hata hawa wanasiasa hawakutuma mchango! Leo mmekuja nini? Mchango mtakaotoa ni unafiki tu,” aliwaka.

Viti viligeuka kuwa moto kwa wengi kutokana na ukweli mchungu uliowachoma huku baadhi ya waliomsaidia mwendazake kabla ya mauko yake wakishangilia kumuunga mkono pasta msema ukweli.

***

Ubadilike au talaka! Jamaa achemkia mke kwa kumtia upweke

MTWAPA MJINI

NA JANET KAVUNGA

BUDA wa hapa ametishia kumtaliki mkewe iwapo ataendelea kumnyima muda wa kuwa naye.

Jamaa alisikitika kwamba anaishi kwa upweke huku mkewe akitumia muda mwingi na marafiki kazini.

“Imekuwa miaka sita sasa ninaishi kwa upweke ilhali niko na mke huku ukitumia muda wako mwingi na marafiki. Hata ukiwa nyumbani unanipuuza na kushinda ukichati na mashoga wako,” aliwaka jamaa.

“Mambo ni mawili; ubadilishe tabia au nikupe talaka,” akamweleza mkewe alipomfuata hadi alikokuwa na marafiki zake wakijivinjari Jumamosi.

Kidosho alinyanyuka akawaacha marafiki na kumfuata mumewe akionekana kujutia tabia yake.

  • Tags

You can share this post!

Amos Rono sasa atangaza kuvunjilia mbali harusi na Nelly...

Mholanzi aliyetupwa rumande kwa madai ya kuchafua watoto...

T L