• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 8:50 AM
Matiang’i chini ya ulinzi mkali

Matiang’i chini ya ulinzi mkali

Na STEVE NJUGUNA

WAZIRI wa Usalama, Dkt Fred Matiang’i alishuhudia madhila yanayowakumba wakazi wa eneo la Ol Moran, majangili walipotekeleza uvamizi na kuteketeza nyumba kadhaa.

Matiang’i aliyezuru eneo hilo chini ya ulinzi mkali alitangaza kuwa kikosi cha polisi kitaanzishwa eneo hilo, polisi wa akiba kuongezwa na kupewa silaha katika juhudi za kukabiliana na vitendo vya ujangili.

Dkt Matiang’i, aliyezuru eneo bunge la Laikipia Magharibi alionekana kushangazwa na mashambulio hayo.

Lakini hata kabla ya kusikiza madhila ya wakazi, nyumba zaidi ziliteketezwa katika kijiji cha Dam Samaki, kilomita chache kutoka eneo ambako alikuwa akikutana na viongozi wa eneo hilo pamoja na wakazi.

Jumla ya nyumba saba ziliteketezwa katika shambulio la jana, zikiwemo nyumba mbili za Polisi wa Akiba.

Hata hivyo, hakuna aliyejeruhiwa katika kisa hicho kwa sababu tayari familia zinazoishi katika eneo hilo zilikwisha kutoroka.

“Walivamia boma zetu Ijumaa (jana) asubuhi na kuwasha moto wakituamuru tuhame,” akasema Mary Maina, mkazi wa kijiji hicho.

You can share this post!

Serikali yabuni kaunti ndogo mpya

Klopp na Pep watofautiana kuhusu pendekezo la Kombe la...