NA WINNIE ONYANDO
GAVANA wa Nairobi Johnson Sakaja amefichua kuwa alikuwa miongoni mwa viongozi walioalikwa kuendesha baiskeli na Mama wa Taifa, Rachel Ruto mwezi Juni lakini akakataa.
Mkewe Rais William Ruto, Bi Rachel, aliendesha baiskeli kutoka Ikulu akapitia kwenye barabara ndani ya msitu wa Karura hadi Gigiri kwa mkutano katika makao makuu ya Mpango wa Mazingira wa Umoja wa Mataifa, mwezi mmoja tu baada ya kuendesha baiskeli kutoka Ikulu hadi Msitu wa Karura ili kuhamasisha umma kuhusu umuhimu wa kukumbatia uendeshaji baiskeli na nyenzo nyingine inayosaidia kuhifadhi mazingira.
Akizungumza katika bustani ya Uhuru Park mnamo Ijumaa baada ya kukutana na wasanii, Gavana Sakaja alifichua kwamba alikataa kushiriki katika zoezi hilo kwa kuwa barabara nchini ni mbovu na zinahitaji kufanyiwa ukarabati.
“Nilitakiwa kuendesha baiskeli na Mkewe Rais hadi Karura lakini nilikataa kwa sababu niliona aibu kuendesha baiskeli katikati ya barabara. Tunafaa kuhakikisha tunaendesha baiskeli kwenye eneo maalum lililotengenezwa na kutengewa waendeshaji baiskeli,” akasema Sakaja.