Na SAMMY WAWERU
Mabustani na majumba ya maduka ya jumla mbalimbali jijini Nairobi na viunga vyake siku ya Krismasi yalikuwa yenye pilkapilka za hapa na pale kufuatia wananchi waliomiminika kujivinjari na kupumzika na familia yao.
Idadi ya waliojitekeza hata hivyo ilikuwa ya chini ikilinganishwa na miaka ya awali, ambapo mabustani hushuhudia umati mkubwa wa watu wasiomudu kuenda mashambani kuungana na jamaa zao.
Licha ya idadi ndogo, wachuuzi wa mapochopo hasa yanayopendwa na watoto walijituma kuhudumia waliojitokeza. Katika majumba ya jumla ya Garden City Mall, Two Rivers Mall na Thika Road Mall familia nyingi zilijitokeza kuwapa raha watoto wao ila kiwango cha watu kilikuwa chini ikilinganishwa na mwaka uliopita.
Bei ya vyakula na vinywaji katika maeneo hayo matatu ilisalia juu, huku watoto wakilazimika kumeza mate tu kwani wazazi wao hawangemudu kuwanunulia.
“Iweje ninunue chakula cha Sh4,000 kwa watoto wangu wawili? Kisha niwapandishe teksi ya Sh2,000 hadi nyumbani. Maisha ni ghali mno na hela hakuna. Ni Krismasi kavu sana. Tutapanda matatu ya kawaida, nitawapikia chakula nyumbani,” akasema Judy Mwongeli aliyezuru enel la Garden City.
Taifa Leo Dijitali ilipozuru mabustani ya Uhuru Park, City Park na Uthiru Ijumaa, wafanyabishara walisema kuwa ingawa watu walijitokeza, hawakuwa na hela za kununua bidhaa za watoto na mapochopocha kwa wingi kama mwaka uliopita.
“Idadi ya watu mwaka huu kwenye mabustani ni ya chini mno. Isitoshe, watu wanalia kukosa pesa, biashara zimeathirika,” Ruth Wambui, mmoja wa wachuuzi wa peremende akasema.
Mkurupuko wa janga la Covid-19 nchini umeathiri sekta nyingi ikiwemo ya biashara, uchukuzi na utalii, hali iliyosabanisha wengi kusalia mijini kwa kukosa nauli ya kusafiri mashambani kuungana na familia zao.
Bustani ya TRM, iliyoko eneo la Roysambu, Thika Road, idadi ya watu ilikuwa ya chini. “Inaonekana wale ambao hawakusafiri wameamua kuadhimishia Krismasi kwenye nyumba. Awali, wakati wa shamrashamra za Sikukuu ya Krismasi huvuna pesa kupitia kazi ya kupiga picha,” akaeleza paparazzi mmoja.
Martha Thuo, mmoja wa waliofika katika bustani ya TRM alisema gharama ya juu ya usafiri ilimlazimisha kusalia Nairobi.
“Ninanotoka Nyeri nauli kipindi hiki imekuwa zaidi ya Sh800, safari ambayo hulipa kati ya Sh250 – 400 ada ya kawaida. Niliamua sitaungana na jamaa zangu mashambani kwa sababu ya pesa kuwa adimu, biashara zimeathirika. Januari karo inanisubiri,” akasema Martha ambaye ni mama wa watoto watatu.
Wahudumu wa matatu nao wameongeza nauli hadi zaidi ya maradufu, huku teksi za kidijitali kama Uber, Bolt na Little Ride nazo zikipandisha nauli mara tatu kwa kuwa ni msimu wa sherehe.