• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 12:09 PM
Yaya aliyewajeruhi watoto wa mwajiri aliyemfuta kazi atiwa mbaroni

Yaya aliyewajeruhi watoto wa mwajiri aliyemfuta kazi atiwa mbaroni

Na SAMMY WAWERU

HATIMAYE yaya aliyeonekana akipiga kikatili watoto wa aliyekuwa mwajiri wake amekamatwa.

Hii ni kufuatia video na picha zilizoonyesha yaya huyo akiwapiga kinyama watoto wawili, wanaosemekana kuwa na umri wa miaka mitano na 11.

Wachangiaji mitandao walisambaza video na picha hizo, za Gladys Naliaka Nalianya, huku wakiihimiza Idara ya Uchunguzi wa Jinai (DCI) kumtia nguvuni na kumchukulia hatua kwa dhuluma aliyotekeleza.

Kulingana na DCI, Gladys alikamatwa Ijumaa adhuhuri, mjini Eldoret akiwa katika harakati za kutorokea nchi jirani, kupitia Busia.

“Alikuwa amekata tiketi ya kuelekea Busia kupitia kampuni ya usafiri na uchukuzi ya Eldoret Express, ambapo alilenga kutorokea nchi jirani inakoaminika ana mizizi,” DCI ikaelezea kwenye taarifa yake kwa vyombo vya habari.

Mshukiwa alipatikana na vitambulisho viwili.

Idara ya Uchunguzi wa Jinai pia imethibitisha watoto hao wachanga wanaendelea kupata matibabu katika hospitali moja jijini Nairobi.

“Hisia zetu pia zilivutiwa na video ya mama ya watoto hao wenye umri wa miaka 5 na 11, aliyopakia mitandaoni akiomba usaidizi kutafuta mshukiwa. Watoto hao wamelazwa hospitalini wakiwa katika hali mbaya, kufuatia majeraha ya kudungwa na kuchapwa,” ikaarifu.

“Tunashukuru umma kwa kutoa taarifa zilizosaidia kumkamata na pia kampuni ya Eldoret Express kwa kushirikiana nasi,” DCI ikasema.

Mshukiwa amefikishwa jijini Nairobi, ambapo amezuiliwa na maafisa wa DCI kwa uchunguzi zaidi na kufunguliwa mashtaka.

Inasemekana alitekeleza unyama kwa watoto hao baada ya kutofautiana na mwajiri na kufutwa.

Duru zinaarifu alirejea siku kadha baada ya kutimuliwa, na kushambulia watoto hao katika mazingira ya boma la mwajiri.

  • Tags

You can share this post!

Obiri ang’ara mbio za mita 10,000

Wahalifu watumia maombi kuwahadaa wakazi wa Thika