• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 10:50 AM
Kisanga kituo cha polisi Nakuru wanaume 2 wakihubiri juu ya mti wakiwa uchi

Kisanga kituo cha polisi Nakuru wanaume 2 wakihubiri juu ya mti wakiwa uchi

NA MERCY KOSKEI

KISANGA kilishuhudiwa Ijumaa katika Kituo Kikuu cha polisi Nakuru, baada ya wanaume wawili kukwea mti wakiwa uchi na kuhubiri.

Kulingana na walioshuhudia, kisa hicho kilitokea wawili hao walipofika na kuvua nguo, wakapanda mti na kuanza kuporomosha injili.

Kabla ya kisanga, inasemekana walifanya jaribio la kwanza mnamo Alhamisi usiku ila jitihada zao zilitibuliwa na maafisa wa polisi waliokuwa wakishika doria.

“Kwa ujasiiri, walipowasili walivua nguo wakapanda mti na kuanza kuhubiri,” Tom Ondigo, mkazi, akaambia Taifa Leo.

Kwa mujibu wa masimulizi ya walioshuhudia, walifika katika kituo hicho asubuhi na mapema bila ufahamu wa polisi.

Wakazi wakifuatilia kisanga ambapo wanaume wawili walipanda mti       wakiwa uchi katika Kituo Kikuu cha Polisi Nakuru na kuhubiri. PICHA / MERCY KOSKEI

Wakazi waliojitokeza, hawakusita kutumia simu zao kunasa matukio ya drama hiyo ya kuvunja mbavu.

Kuhubiri wakiwa uchi

Mojawapo ya video iliyonasa matukio, inaonyesha wakihubiri juu ya mti wakiwa uchi.

Isitoshe, bila wasiwasi wanaonekana wakiendelea kunukuu vifungu vya Biblia.

Kamanda wa Polisi Kaunti Ndogo ya Nakuru Mashariki, Martin Masika, aliambia Taifa Leo kwamba waliwafumania asubuhi wakihubiri wakiwa uchi, wakiwa wamevalia chupi pekee.

Jitihada zetu kuwarai kushuka hata hivyo ziliambulia patupu, Bw Masika alisema.

“Tulipowauliza maswali wakiwa mtini kuelewa kilichowasukuma kufanya hivyo, mambo yalizidi unga na kuvuta umati mkubwa wa watu. Tulikuwa makini wasije wakaanguka na kusababisha hasara ya majeraha au hata maafa,” alielezea.

Kushuka jioni

Cha kushangaza, waliitikia kuteremka kutoka kilele cha mti waliokwea saa tisa na nusu jioni baada ya umma kuwabembeleza.

“Hawakufichua sababu za kufanya tendo la aina hiyo katika kituo cha polisi,” afisa huyo akasema, akionekanaa kushangazwa na drama hiyo yenye ucheshi.

Wakazi wakishuhudia drama wanaume wawili walipopanda mti wakiwa uchi katika Kituo Kikuu cha Polisi Nakuru na kuhubiri. PICHA / MERCY KOSKEI

Felix Kiprono, mwendesha bodaboda, alisema alishtuka kukuta kioja hicho kikifanyikia mita chache kutoka eneo analohudumu.

“Hata ingawa hatua waliyochukua si sahihi, huenda hali ngumu ya maisha iliwachochea. Kilikuwa kioja cha kufurahisha lakini,” Kiprono akasema.

Umati wa watu waliojitokeza kushuhudia, ulisababisha msongamano wa magari katika barabara ya Jaramogi Oginga Odinga.

Haikubainika ni kwa nini wawili hao waliamua kusababisha drama nje ya kituo cha polisi, picha za tukio hilo zikiendelea kuzua gumzo na ucheshi mitandaoni.

[email protected]

  • Tags

You can share this post!

WANDERI KAMAU: Kwa kuwatoza ‘mama-mboga na boda’ ada...

Mchanga wa ufuoni unavyotia ladha njugu

T L