• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 11:29 AM
ODM wamchoka Owalo na misaada yake ya chakula Luo Nyanza

ODM wamchoka Owalo na misaada yake ya chakula Luo Nyanza

Na GEORGE ODIWUOR

MAAFISA wa ODM wameshtumu hafla za Waziri wa Teknolojia na Mawasiliano Eliud Owalo ambaye amekuwa akipiga kambi eneo la Luo Nyanza akisambaza chakula cha msaada.

Viongozi hao wa ODM wamemkashifu Bw Owalo kwa kutumia hafla hizo za kusambaza vyakula kujaribu kummaliza kisiasa kiongozi wa ODM Raila Odinga. Wanadai hiyo ni mbinu yake ya kujitafutia umaarufu ndani ya serikali ya Kenya Kwanza.

Kwa mujibu wa Kiongozi wa Wachache kwenye Bunge la Kitaifa Opiyo Wandayi, wakazi wa Nyanza hawahitaji chakula cha msaada na w Bw Owalo anastahili asitishe shughuli hizo za kusambaza chakula.

“Hatupingi kusambazwa kwa chakula. Hata hivyo, huwezi kuwapa watu chakula kisha kutaka wabadilishe misimamo yao ya kisiasa,” akasema Bw Wandayi.

Tangu achaguliwe Waziri, Bw Owalo amekuwa akizuru kaunti nne za Luo Nyanza ili kusambaza vyakula vya misaada kwa familia zisizojiweza. Pia amekuwa akirai jamii ya Waluo iiunge mkono utawala wa Kenya Kwanza.

Ingawa hivyo, kwenye hotuba zake nyingi amekuwa akikwepa sana siasa na kumakinikia mipango ya serikali ya Kenya Kwanza na miradi inayopanga kukumbatia eneo hilo.

Hata hivyo, wanasiasa ambao wamekuwa wakiandamana na Bw Owalo wamekuwa wakitaja hadharani kuwa jamii ya Waluo inastahili kubadili fikira na kukoma kuunga mkono Kinara wa Azimio Raila Odinga.

Mnamo Ijumaa, Bw Owalo alikuwa katika kisiwa cha Mfang’ano, Homa Bay kisha akafululiza hadi Kaunti ya Migori kusambaza vyakula vya misaada. Alikuwa ameandamana na Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Bw Owalo alijitetea akisema kuwa kusambazwa kwa chakula cha msaada ni sehemu ya mpango wa Rais kuwaokoa Wakenya ambao wanakabiliwa na njaa.

“Tuna mipango ya kuinua Nyanza kiuchumi ikiwemo kufufua uchukuzi wa ziwani, kuwainua wavuvi wetu na kubuni nafasi za ajira. Haya yote yatawezekana iwapo tutakubali kushirikiana na utawala wa sasa,” akasema Bw Owalo akiwa Nyatoto, Suba.

Ingawa hivyo, Bw Wandayi alisema kuwa chakula kinachosambazwa na Bw Owalo ni kidogo na hakiwezi kukimu familia. Bw Wandayi alisema nia ya waziri huyo ni kugawanya Nyanza akiwatumia wanasiasa ambao ni wasaliti na walikuwa ODM.

  • Tags

You can share this post!

Mwanamke anayedai ni binti ya Mvurya ataka alipiwe karo

Mackenzie hubomoa chakula sawasawa akiwa kizuizini,...

T L