• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
Papa Francis aendelea kupata nafuu baada ya kulazwa

Papa Francis aendelea kupata nafuu baada ya kulazwa

NA MASHIRIKA

ROMA, ITALIA

KIONGOZI wa kanisa katoliki Ulimwenguni, Papa Francis alilazwa hospitalini mnamo Jumatano kutokana na maambukizi ya mapafu.

Taarifa kutoka makao makuu ya Papa jijini Vatican ilisema hayo baada ya kiongozi huyo kukabiliwa na matatizo ya kupumua katika siku za hivi karibuni.
Aliongeza kwamba atakaa hospitali kwa siku kadhaa akipokea matibabu.

Kuhusu ikiwa Papa Francis amekuwa akiugua Corona, Msemaji wa Vatican, Matteo Bruni amesema katika taarifa kwamba Papa, mwenye umri wa miaka 86, alikanusha na kusizitiza kwamba Papa hana Corona.

Hii ni mara ya kwanza kwa Francis kulazwa hospitalini tangu alipolazwa siku 10 katika hospitali ya Gemelli mwezi Julai mwaka wa 2021 na kufanyiwa upasuaji kwenye matumbo.

Maswali yameibuka kuhusu hali ya afya ya Francis na uwezo wake kusherehekea matukio mengi ya wiki takatifu ambayo inaanza mwishoni mwa wiki hii kwa kuwa ni Jumapili ya Matawi.

Hapo awali, Matteo alisema Papa huyo amelazwa katika hospitali ya Gemelli ya Roma kwa ajili ya vipimo vilivyopangwa awali – lakini katika taarifa ya baadaye ilifichua kwamba Francis alilalamika katika siku zilizopita za “kupumua kwa shida.”

Uchunguzi ulionyesha maambukizo ya kupumua ambayo hayakuwa Covid-19, yanayohitaji “alazwe hospitalini kwa siku siku chache akipata matibabu mwafaka”, msemaji wa Vatican Matteo Bruni alisema.

Mdokezi kutoka Vatican aliambia shirika la habari la AFP kwamba ratiba ya shughuli za Papa za Alhamisi asubuhi ilisimamishwa.

Kulazwa kwa Francis – ambako kulifanya waandishi wa habari kadhaa kukita kambi nje ya hospitali Jumatano usiku – kunajiri wiki chache baada ya kuadhimisha muongo mmoja kama mkuu wa Kanisa Katoliki.

Isitoshe, inajiri kabla ya Wiki Takatifu na Pasaka, likizo muhimu zaidi ya Ukristo.
Katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, Francis amekuwa na maumivu makali ya goti ambayo yalimlazimu kutumia kiti cha magurudumu.

Kuahirishwa kwa ziara yake iliyopangwa kufanyika barani Afrika na matukio mbalimbali ya nyumbani kulichochea uvumi mkubwa kuhusu afya yake.

Aidha, katika mahojiano na wanahabari mnamo Julai 2022, alikiri kwamba alihitaji kupunguza kasi.

Alionekana wakati huo akiwa mchangamfu siku hiyo.
Kadhalika, katika mkutano wake wa kila wiki mjini Vatican, mnamo Jumatano asubuhi, papa alionekana amechangamka, akitabasamu alipokuwa akiwasalimu waumini kutoka kwa “popemobile” yake.
Hata hivyo, alionekana akitabasamu huku akisaidiwa kuingia kwenye gari.

  • Tags

You can share this post!

Raila alaani uvamizi katika shamba la Uhuru Ruiru

Mwadime akosolewa kwa kuajiri washauri 7

T L