• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 5:01 PM
KINA CHA FIKIRA: Ujeuri wa mpapai hujeruhi na udhalili wa unyasi huokoa

KINA CHA FIKIRA: Ujeuri wa mpapai hujeruhi na udhalili wa unyasi huokoa

Na WALLAH BIN WALLAH

KILA mwanadamu ana hulka au tabia tofauti.

Wapo wenye tabia za upole, unyenyekevu na heshima.

Pia wapo wenye tabia za ujeuri, ukali, hasira na kiburi!

Watu wenye sifa za ujeuri na kiburi hujisifu wakidhani ati ujeuri ni ushujaa!

Wanasahau kwamba kujisifu au kusifiwa kwa kufanya vitendo vya ujeuri, ukatili na kiburi ni kashfa wala si sifa njema!

Hawakumbuki methali zisemazo, ‘Kwa shujaa huenda kilio, kwa mwoga huenda kicheko; na kiburi si maungwana?’

Unyenyekevu na heshima huambatana na woga! Mtu mtiifu mwenye nidhamu huwa mwoga!

Kamwe hajipigi kifua hadharani na kujigamba au kujionyesha kiburi chake kama sokwe dume!

Chunguza nukuu za vitabu vya dini zote wanasema, ‘Ogopa Mungu wako!’

Yaani uwe mnyenyekevu na mtiifu kwa Mungu wako! Woga ni heshima! Hapo ndipo nilipopata ari na hamasa ya kuandika kauli ya leo katika Kina cha Fikira!

Babu yangu Mzee Majuto alikuwa mkulima na mfugaji maarufu.

Shambani kwake kulikuwa na mpapai mkubwa uliozaa mapapai mengi makubwa! Karibu na mpapai huo kulikuwa na nyasi ndefu zilizostawi kuwa chakula cha ng’ombe wake!

Siku moja jioni mawingu mazito meusi yalitanda ghafla angani! Mara upepo mkali ukaanza kuvuma na ngurumo za radi kurindima kuashiria mvua kubwa!

Hatimaye mvua kubwa ya theluji ikaanza kumwagika! Watu wote wakajifungia ndani ya nyumba zao. Nyasi zile ndefu zilizokuwa karibu na mpapai zikalala chini ardhini kwa kuogopa hasira za upepo na kani za mvua kubwa! Lakini mpapai ule mkubwa ulisimama tu kwa kiburi na ujeuri bila kuogopa wala kuinama kuepuka dhoruba ya mvua!

Mvua ilipozidi kumwagika na upepo kuvuma zaidi, mpapai ulivunjika matunda yake yote yakapukutika chini!

Asubuhi kulipokucha kulikuwa shwari baada ya mvua kupusa. Nyasi zile zilianza kunyanyuka taratibu na kusimama kuendelea kuishi kama kawaida!

Mpapai uliovunjika ulipoona nyasi zikisimama tena, mpapai ukafoka, “Mbona nyinyi nyasi na unyonge wenu hamkuvunjika kama mimi mpapai ilhali nina nguvu na thamani zaidi yenu?”

Nyasi zilijibu kwa upole, “Wewe mpapai umeanguka ukavunjika kwa sababu ya ujeuri wako na kiburi chako! Sisi nyasi na unyonge wetu tuliogopa upepo mkali na mvua kubwa tukanyenyekea tukalala chini kwa heshima mpaka tufani ilipoisha! Tumenusurika!”

Ndugu wapenzi, tuwe watu wanyenyekevu wenye nidhamu ili tuepuke majanga tuishi maisha marefu!

Ujeuri hujeruhi na unyenyekevu huokoa maisha! Unyenyekevu wa unyasi ndio usalama wa unyasi! Nimewaambia!!!!!

You can share this post!

SAUTI YA MKEREKETWA: Sekta ya elimu nchini itafaidi iwapo...

NASAHA: Fanya uamuzi wa dhati kuhusu taaluma uitakayo...