• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 5:01 PM
KINA CHA FIKIRA: Uzuri na ubaya wa mtu umo ndani ya mtu mwenyewe!

KINA CHA FIKIRA: Uzuri na ubaya wa mtu umo ndani ya mtu mwenyewe!

Na WALLAH BIN WALLAH

SIFA za upole na ujeuri zimefichamana ndani ya mtu!

Hazionekani mpaka zichokorwe na kuchokozwa ndipo zilipuke kama bomu au guruneti lililokanyagwa njiani! Kila mwanadamu ana ubora na unyonge wake. Ana wema wake na chembechembe za uovu wake ndani kwa ndani! Lakini wema na uzuri hupaliliwa na kukuzwa ili mtu awe bora kabisa! Aidha ubaya au uovu na ujeuri hudekezwa mpaka mtu akawa mjeuri sugu wa kuwaogofya wengine! Ni wajibu wetu sisi sote katika jamii kutoa miongozo ya kuwalea watoto wetu huku tukijiuliza, “Tunawaelekeza upande wa kuwa waovu au waadilifu?”

Mageugeu alikuwa kijana mdogo mwanafunzi wa gredi ya nne katika shule ya Kijiweni. Alijulikana kwa ujeuri wake tu! Wanafunzi wenzake walimkemea kila mara, “Wewe Mageugeu u mjeuri mno!” Walimu nao walimshutumu, “Wewe mtoto mbaya sana! Badilika uwe mwema na mpole! Uwe mtoto mzuri!” Lawama zote hizo zilimkera Mageugeu moyoni! Kila jioni alirudi nyumbani ameudhika na kununa! Mama yake aliona tabia hiyo siku nyingi. Jumamosi moja, alimwambia mwanawe, “Wewe Mageugeu una roho mbaya sana! Wewe mtoto mbaya zaidi! Huna furaha wala husemi na wenzako! Tabia mbaya hii umetoa wapi?”

Mageugeu alimjibu mama kwa hasira, “Watu hawanitaki wala hawanipendi! Shuleni kila mtu ananiita mtoto mbaya! Tena nyumbani hapa mamangu unaniita mtoto mbaya!? Basi mimi sina hamu ya kuishi! Heri nikajinyonge!!” Akachukua kamba akaenda kwenye mabonde ya milima ya kwao! Akalia kwa kelele, “Mimi mbaya!! Mimi mbaya aa!!” Alishtuka aliposikia sauti kubwa ikisema kutoka milimani, “Mi-mi mba-mbaya!!” Mi-mi mba-mbayaa-aa-aa!!” Mageugeu alitoka mbio na kamba mkononi kurudi nyumbani kumwomba mama msamaha! Akasema, “Mama unisamehe! Leo nimeamini mimi mbaya! Milima na watu wote wa mabonde huko wamesema kwa sauti, “Mimi mbaya!!” Kumbe siyo chuki! Mimi ni mbaya kweli! Sasa naenda kujinyonga kwa sababu ya ubaya wangu! Nimemsamehe kila mtu!”

Mama alijua kwamba Mageugeu alisikia mwangwi! Akamshauri kwa upole, “Kabla hujajinyonga huko, uende upige kelele useme, “Mimi mzuriiiiiiiiiii!!” Mageugeu alifika mabondeni akapiga kelele, “Mimi mzuriiiiiiiiiii!!!” Sauti ilirejelea, “Mimi mzuriiiiiiiiiii iii iii!!!” Alishangaa akarudi nyumbani kumwambia mama, “Sasa wamesema mimi mzuri!” Mama alimjibu, “Naam, mwanangu, umekuwa mzuri! Watu wa milimani wamekubali wewe mzuri! Na uwe mzuri sana kuanzia leo! Usiwe mbaya tena!”

Ndugu wapenzi, Mageugeu alibadilika akawa mtoto mwema sana! Uzuri na ubaya wa mtu umo ndani ya mtu! Ukikubali kuwa mwema utakuwa mwema tu! Uamuzi ni wako!!!!

You can share this post!

WASONGA: Viongozi wajadili masuala yanayoathiri raia moja...

Madiwani wavuna baada ya SRC kuidhinisha kila mmoja apewe...