• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 10:50 AM
TAHARIRI: Shule zisiwafukuze wanafunzi kiholela

TAHARIRI: Shule zisiwafukuze wanafunzi kiholela

KITENGO CHA UHARIRI

WANAFUNZI wanapofungua shule hapo Jumanne, wazazi wengi wanakabiliwa na mzigo mzito wa kulipa karo.

Mzigo mzito hasa ikizingatiwa kuwa muhula wa kwanza ulikamilika siku 10 tu zilizopita.

Kutokana na ufupi wa muhula huo, kuna uwezekano mkubwa kuwa wazazi wengi hawakumaliza kulipa karo ya muhula huo, au wengine waliomaliza walifanya hivyo katika siku za mwisho mwisho za muhula.

Kutokana na hali hiyo, ni muhimu serikali kupitia kwa Wizara ya Elimu iingilie kati kwa kuzikataza shule na walimu wakuu kuwafukuza wanafunzi mwanzoni mwa muhula.

Ni kweli kuwa kila mzazi au mlezi anafaa kujitahidi kulipa karo ya shule.

Hata hivyo, ni bayana kuwa wapo baadhi ya wazazi au walezi ambao huenda wakalemewa kukamilisha ada hiyo mapema jinsi inavyohitajika hasa kutokana na makali ya janga la Covid-19.

Jinsi ya kuwasaidia wazazi hao ni kuwapa muda wa kutosha kukamilisha malipo hayo bila kuwafukuza watoto wao wasije wakakosa masomo.

Hiyo itasaidia pande zote kunufaika kwani shule zitapata pesa kuendeshea shughuli za masomo nao wanafunzi watasoma bila kukosa kipindi chochote.

Ili kufanikisha hilo, serikali inahitajika kutoa mwelekeo kwa shule kuwavumilia wazazi watakaoshindwa kuwalipia watoto wao ada za shule hasa kwa kuzingatia hali ngumu ya uchumi iliyoko sasa.

Kwa upande mwingine, wazazi nao wahimizwe kutozembea katika utafutaji wa pesa za kulipa karo.

Kauli hii inahusu hasa shule za upili, vyuo na shule zote za kibinafsi zinazohitaji malipo ya karo.

Inapozingatiwa pia kuwa muhula umepungua kwa zaidi ya mwezi mmoja, zipo baadhi ya ada kama vile chakula cha wanafunzi na michezo zinazohitajika kupunguzwa ili kuwapa wazazi nafuu ya mzigo huo.

Mbali na masuala ya karo, itakuwa muhimu shule na wadau wakuu hasa Wizara ya Elimu kuhakikisha kuwa wanajitahidi kufundisha sehemu kubwa ya silabasi.

Inafahamika kuwa uwezo wa binadamu kunasa mambo mengi akilini kwa muda mfupi ni mdogo, lakini ipo haja ya kutumia muda huo mfupi kuhakikisha wanafunzi wananasa mambo mengi iwezekanavyo ya kielimu.

Huenda pia ikawa muhimu kupunguza majaribio ya mitihani ili muda huo uweze kutumiwa kufundisha kwa dhamira ya kukamilisha silabasi ambayo kwa kawaida inafaa kumalizika katika muda wa miezi tisa badala ya sita ya sasa, kwa mwaka.

You can share this post!

DINI: Furaha imo katika kumaliza kila unachopanga kufanya...

JAMVI: Huyu atakayembwaga Ruto Mlimani ni nani?