• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
ZARAA: Mfumo ulioboreshwa kuendeleza kilimo mijini

ZARAA: Mfumo ulioboreshwa kuendeleza kilimo mijini

NA SAMMY WAWERU

MOJAWAPO ya ajenda kuu za serikali ni kukabiliana na kero ya uhaba na usalama wa chakula nchini. 

Hata ingawa kuidhinishwa kwa uagizaji bidhaa za GMO kumezua mjadala moto, Waziri wa Biashara Moses Kuria mwishoni mwa wiki iliyopita alitangaza kuanza kununuliwa nje mahindi yaliyoboreshwa kupitia mfumo huo tata.

Akitetea uamuzi huo, Waziri Kuria alisema “ni jukumu la serikali kuhakikisha kila Mkenya anapata chakula”.

Mifumo ya teknolojia kuendeleza kilimo inapigiwa upatu kuchangia uzalishaji wa chakula.

Mbali na maeneo ya mashambani kuwa kapu la mazao, miji inalengwa kupitia mabustani.

Zipo mbinu ainati kugeuza mabustani hayo kuwa uga wa kilimo cha kisasa mojawapo ikiwa matumizi ya shamba garden units.

Ni mfumo wa paipu za plastiki zilizounganishwa, na kupandwa mseto wa mboga, viungo vya mapishi na matunda.

Zile tajika zikiwa vertical gardens, Wilson Njuguna mwasisi wa Lavington Herbs amevumbua muundo ulioboreshwa.

Wilson Njuguna mwanzilishi Lavington Herbs, akionyesha mseto wa mboga na viungo vya mapishi vilivyopandwa kwenye semi-permanent tower garden. PICHA | SAMMY WAWERU

Kampuni yake inashughulika na uzalishaji wa miche ya matundaasilia, viungo, na vifaa tamba vya kisasa kuendeleza kilimo mijini.

Akitambua muundo aliovumbua kama semi-permanent tower garden, anasema nafasi mbadala ya shamba inayohitajika ni kidogo, matumizi ya maji yakiwa yamedhibitiwa na rahisi kukabiliana na wadudu na magonjwa.

“Isitoshe, muundo huu mpya mkulima anavuna kiwango cha mazao anayohitaji kula au kuuza. Hivyo basi, unapunguza utupaji na uharibifu wa chakula,” Njuguna adokeza.

Mfumo huo aidha unawafaa wakazi wa mijini, vifaa hivyo vikiwekwa kwenye kuta, kando ya njia za magari na kwenye maegesho.

Kando na kuwa bora kukuza mseto wa mboga, Njuguna ambaye pia ni mkulima anasema ni faafu kulima matunda kama matikitimaji, stroberi na karakara.

Hali kadhalika, nyanya, vitunguu, biringanya, dhania na pilipili mboga.

Ikiwa imeundwa kwa paipu aina ya PVC, semi-permanent tower garden huunganishwa kwa nyaya kusaidia kusitiri mimea inayotambaa kuelekea juu.

Semi-permanent tower garden kwenye bustani. PICHA | SAMMY WAWERU

Mvumbuzi huyo anasema muundo unapatikana kwa saizi ndogo; yenye urefu wa futi 4.5, ya kadri 5 na kubwa 7, yote ikiwa na upana wa futi 1 mraba sakafuni.

Kulingana na Njuguna, ndogo inakuzwa kati ya mimea 15 – 18, kadri 24 na kubwa 30.

“Ni mfumo unaodhibiti matumizi ya maji kwa kiwango kikuu. Mfano, muundo mmoja unaweza kutumia lita moja kwa siku badala ya 20 mimea iliyopandwa shambani,” aelezea, akitaja mboleaasilia, ya mifugo, pumice (unga unaotokana na mawe ya Volkeno) na udongo, kama kipandio baada ya kuchanganya vyema.

Kwenye bustani, vifaa hivyo vinawekwa umbali wa futi moja.

Joash Njani, mtaalamu masuala ya kilimo anataja mifumo ya aina hiyo kama mbinu bora zaidi kujumuisha maeneo ya miji kuchangia uzalishaji chakula.

“Mabadiliko ya tabianchi ambayo yamechangia janga la ukame, yametufunza tugeuze miji kuwa kijani.

“Mifumo ya mabustani ya plastiki ni kati ya mbinu tunazopaswa kukumbatia kuongeza kiwango cha chakula nchini,” mdau huyo ashauri.

  • Tags

You can share this post!

KOMBE LA DUNIA FIFA 2022: Canada waaga kipute katika hatua...

Coe afurahia juhudi za Kenya kuimarisha vita dhidi ya pufya

T L