Na MASHIRIKA
ARSENAL walifungua pengo la alama nne kileleni mwa jedwali la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) hapo jana baada ya kupepeta watani wao Tottenham Hotspur 3-1 uwanjani Emirates.
Masogora hao wa kocha Mikel Arteta walitamalaki mchezo kuanzia mwanzo na wakapata mteremko zaidi katika kipindi cha pili baada ya Emerson Royal wa Spurs kuonyeshwa kadi nyekundu kwa hatia ya kumchezea Gabriel Martinelli visivyo.
Mabao ya The Gunners yalifumwa wavuni kupitia Thomas Partey, Gabriel Jesus na Granit Xhaka. Spurs ya mkufunzi Antonio Conte ilifutiwa machozi na Harry Kane kupitia penalti iliyochangiwa na Gabriel Magalhaes aliyemwangusha Richarlison Andrade ndani ya kijisanduku.
Bao la Kane lilikuwa lake la 14 kutokana na mechi 18 dhidi ya Arsenal katika EPL na la 100 ambalo amelipata katika ligi ugenini. Miamba hao sasa wanadhibiti kilele cha jedwali kwa alama 21, nne zaidi kuliko Spurs na mabingwa watetezi Manchester City watakaoalika Manchester United ugani Etihad mnamo Oktoba 2, 2022.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO