• Nairobi
  • Last Updated May 21st, 2024 8:55 PM
Benfica watandika Club Bruges katika UEFA ugenini na kujiweka pazuri kutinga robo-fainali za kipute hicho

Benfica watandika Club Bruges katika UEFA ugenini na kujiweka pazuri kutinga robo-fainali za kipute hicho

Na MASHIRIKA

BENFICA waliweka hai matumaini ya kutinga robo-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) msimu huu wa 2022-23 baada ya kutandika Club Bruges ya kocha Scott Parker 2-0 katika mchuano wa mkondo wa kwanza wa hatua ya 16-bora mnamo Jumatano usiku nchini Ubelgiji.

Jack Hendry aliangusha Goncalo Ramos ndani ya kijisanduku mwanzoni mwa kipindi cha kwanza na kumpa Joao Mario fursa ya kufunga penalti ambayo nusura ipanguliwe na kipa Simon Mignolet.

David Neres alifunga bao la pili la Benfica dakika mbili kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mchezo kupulizwa.

Parker, aliyeanza kudhibiti mikoba ya Bruges mnamo Disemba, sasa ana mtihani mgumu wa kubatilisha ushindi wa Benfica watakaokuwa wakichezea mbele ya mashabiki wao wa nyumbani jijini Lisbon, Ureno mnamo Machi 7, 2023.

Hii ni mara ya kwanza kwa Bruges kunogesha hatua ya muondoano ya UEFA na walitamalakiwa katika takriban idara zote na Benfica waliopiga kumbo Paris Saint-Germain (PSG) na kumaliza kampeni za makundi kileleni mwa Kundi H kwa alama 14. Kundi hilo lilijumuisha pia Juventus na Maccabi Haifa waliojizolea alama tatu kila mmoja.

Bao la Neres ambaye ni raia wa Brazil lilikuwa la 18 kufungwa na Benfica katika kampeni za UEFA msimu huu wa 2022-23.

Kichapo kutoka kwa Benfica kinamaanisha kuwa kocha Parker sasa ameongoza waajiri wake Bruges kushinda mechi moja pekee kati ya nane ambazo amezisimamia tangu aajiriwe na kikosi hicho.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Bayern Munich wakomoa PSG katika mkondo wa kwanza wa...

AC Milan wazamisha chombo cha Spurs katika gozi la UEFA...

T L