• Nairobi
  • Last Updated May 21st, 2024 8:55 PM
Borussia Dortmund wapepeta Chelsea 1-0 katika hatua ya 16-bora ya UEFA uwanjani Signal Iduna Park

Borussia Dortmund wapepeta Chelsea 1-0 katika hatua ya 16-bora ya UEFA uwanjani Signal Iduna Park

Na MASHIRIKA

BAO la kipindi cha pili kutoka kwa Karim Adeyemi liliwapa Borussia Dortmund ushindi wa 1-0 dhidi ya Chelsea katika mchuano wa mkondo wa kwanza wa hatua ya 16-bora ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Jumatano usiku ugani Signal Iduna Park, Ujerumani.

Chini ya kocha Graham Potter, Chelsea walipoteza nafasi nyingi za wazi za kufunga wenyeji wao katika vipindi vyote viwili vya mchezo huku sajili mpya Joao Felix akishuhudia kombora lake likigonga mwamba wa goli la Dortmund.

Reece James na Enzo Fernandez nao walimwajibisha vilivyo kipa wa Dortmund, Gregor Kobel, katika kipindi cha pili. Bao la Adeyemi lilikuwa zao la ushirikiano kati yake na Emre Can aliyetatiza pakubwa beki Kalidou Koulibaly na kipa Kepa Arrizabalaga.

Kichapo hicho kinaacha kocha Potter katika kibarua kizito cha kusajili ushindi wa angalau mabao 2-0 katika mkondo wa pili wa hatua ya 16-bora mnamo Machi 7, 2023 uwanjani Stamford Bridge.

Hata hivyo, alizidi kulaumiwa kwa maamuzi ya kutoshinikiza waajiri wake kununua fowadi mzoefu na badala yake kikosi hicho kikamwaga mabilioni ya fedha sokoni kwa ajili ya wachezaji wa safu ya kati wakiwemo Mykhailo Mudryk, Fernandez na Felix.

Dortmund walishuka dimbani wakijivunia kushinda mechi zao zote sita zilizopita katika mashindano yote. Kwa upande wao, Chelsea sasa hawajafunga zaidi ya bao moja katika mchuano wowote tangu mwanzo wa Novemba 2022.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Raila kutumia pia maombi kukabili KKA

Man-City watandika Arsenal 3-1 ugani Emirates na kutua...

T L