• Nairobi
  • Last Updated May 15th, 2024 8:55 PM
Club Bruges yakomoa Atletico na kutia guu moja ndani ya hatua ya 16-bora ya UEFA

Club Bruges yakomoa Atletico na kutia guu moja ndani ya hatua ya 16-bora ya UEFA

Na MASHIRIKA

CLUB Bruges walipiga hatua kubwa katika vita vya kutinga hatua ya 16-bora ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) msimu huu kwa kutandika Atletico Madrid 2-0 katika pambano la Kundi B lililowakutanisha nchini Ubelgiji mnamo Jumanne usiku.

Kikosi hicho sasa kina alama tisa kutokana na mechi tatu baada ya kucharaza Bayer Leverkusen na FC Porto katika michuano miwili ya ufunguzi wa Kundi B.

Ferran Jutgla aliwazidi ujanja mabeki kadhaa wa Atletico kabla ya kutoa krosi iliyojazwa kimiani na Kamal Sowah kunako dakika ya 36.

Mhispania Jutgla alifunga bao la pili la waajiri wake baada ya kumegewa krosi na Tajon Buchanan katika dakika ya 62.

Antoine Griezmann, aliyekuwa akichezea Atletico kwa mara ya pili muhula huu, alipoteza mkwaju wa penalti iliyogonga mwamba wa lango la wenyeji wao.

Club Bruges, wanaonolewa na beki wa zamani wa Stoke City na West Bromwich Albion, Carl Hoefkens, kwa sasa wanajivunia pengo la alama sita kileleni mwa Kundi B. Mgongo wao unasomwa na Atletico, Porto na Leverkusen.

Porto walitandika Leverkusen 2-0 katika pambano jingine la Kundi B mnamo Jumanne usiku. Mabao yao katika mechi hiyo iliyochezewa nchini Ureno, yalifumwa wavuni kupitia kwa Zaidu Sanusi na Galeno.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Liverpool wacharaza Rangers 2-0 katika gozi la UEFA ugani...

TAHARIRI: Tutahadhari tukikumbatia vyakula hivi vya GMO

T L