Na MASHIRIKA
KOCHA Julian Nagelsmann amewataka wanasoka wake kuwa “wazalendo na kucheza kwa heshima ya nembo ya kikosi kwenye jezi wanazovalia”.
Hii ni baada ya mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga) kupetetwa 3-1 na Mainz ugenini mnamo Jumamosi.
Bayern walishuka ugani kwa ajili ya mechi hiyo siku chache baada ya kujizolea taji la Bundesliga kwa mara ya 10 mfululizo. Wangalifungwa mabao zaidi na Mainz walioshuhudia makombora yao manne yakigonga mwamba wa lango la wageni wao.
“Tumekosa utashi na msukumo wa kuchezea kikosi. Kikosi hakikujituma jinsi nilivyotarajia au kutazamiwa na mashabiki,” akasema mkufunzi huyo wa zamani wa RB Leipzig.
“Tumeshindwa katika mechi nyingi msimu huu na tumepoteza mechi hizo kwa namna inayoelekea kufanana,” akaongeza Nagelsmann.
Mvamizi raia wa Ujerumani, Jonathan Burkardt na beki wa Ufaransa, Moussa Niakhate, waliwapa Mainz uongozi wa 2-0 kufikia dakika ya 27. Ingawa Robert Lewandowski alirejesha Bayern mchezoni kunako dakika ya 33, Mainz walifunga bao la tatu kupitia kwa Leandro Barreiro kunako dakika ya 57.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO